DAVIES MOSHA KUWAMWAGIA MATOTI WACHEZAJI YANGA

ALIYEKUWA Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Davis Mosha amefurahia ushindi wa bao 1-0, ambao timu hiyo iliupata jana dhidi ya mahasimu wao, Simba SC na kuahidi kuwapa zawadi ya fedha wachezaji.
Mosha aliyezungumza jana kutoka Australia alipo kwa sasa, alisema kwamba ushindi huo umemfurahisha kama mpenzi na mwanachama wa Yanga.
“Naahidi nikirudi nitakutana na wachezaji wote wa timu yangu na kuwapa donge nono kama pongezi kwa ushindi huu,”alisema Mosha.
Hata hivyo, Mosha ambaye alijiuzulu Yanga kutokana na kutoelewana na Mwenyekiti wake Lloyd Nchunga alisema fedha hizo atataka ziwafikie moja kwa moja wachezaji na kupitia kwa kiongozi yoyote.
Lakini Mosha hakusema atarejea lini na atawakabidhi lini wachezaji zawadi hiyo. Yanga juzi ilijiimarisha katika mbio za kutetea ubingwa wa Ligi Kuu ya Bara, baada ya kuwafunga watani wao Simba 1-0, bao pekee la Mzambia Davies Mwape dakika ya 72.
Ushindi huo umeifanya Yanga ifikishe pointi 24 baada ya kucheza 12 na sasa inazidiwa kwa pointi tatu tu na Simba inayoongoza ligi hiyo kwa pointi zake 27.
Yanga itamaliza mzunguko wa kwanza wa ligi kwa kucheza Polisi Tanzania mjini Dodoma Novemba 2, wakati Simba watamaliza na Moro United, Dar es Salaam siku hiyo.

Comments