BENDTNER AMTOLEA UVIVU WENGER

MCHEZAJI Nicklas Bendtner ambaye ameondolewa Arsenal na kupelekwa kwa mkopo Sunderland, ameamua kumpasha kocha wake Arsene Wenger na kumwambia amtoe kabisa katika hesabu kwani hataki kurudi tena katika timu hiyo. Bendtner amepelekwa kwa mkopo wa muda mrefu katika siku ya mwisho ya usajili, baada ya jitihada zake za kuhakikisha anapata mkataba na timu ya kueleweka kuwekewa vikwazo vya kila aina.
Kuondoka kwa Bendtner na kiupelekwa Sunderland kwa mkopo, pia kumewachukiza baadhi ya mashabiki wa Arsenal ambao wanaona kitendo cha kumuondoa hapo hakikuwa sawa, kwani alikuwa bado anahitajika.
“Nachotaka kusema wazi ni kwamba sitarudi tena Arsenal, yaani kama ni kufuata njia yangu, nasema sitaki kuichezea tena timu hiyo chini ya Wenger,” alisema.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Denmark, alimlaumu Wenger pia kwa kutompa nafasi ya kucheza na hasa alipopata ajali ya gari miaka miwili iliyopita. “Baada ya ajali ya gari nikajikuta sipewi tena nafasi ya kucheza, hivi sasa ni mwaka mmoja na nusu sipewi nafasi ya kueleweka, kwa sasa naenda Sunderland lakini msimu ujao ni lazima nijiondokee. “Nitahakikisha Napata timu mpya, lakini sio kurudi Arsenal, hili nina uhakika nalo.”

Comments