WALIOMTEKA BABA OBI WATAKA NAIRA MILIONI 20 KUMUACHIA

Obi akiwa Essien kushoto
Wateka nyara waliomchukua baba wa mchezaji wa Chelsea Jon Obi Mikel wametoa madai ya kutaka 'kiasi kikubwa' cha fedha za kikombozi, amethibitisa wakala wa mchezaji huyo.
Lakini wakala huyo, kampuni ya SEM imekanusha taarifa kutoka kwa polisi wa Nigeria waliosema kiasi hicho ni naira milioni 20, takriban pauni elfu 80.
"Madai ya kiasi kikubwa yametolewa, lakini kwa sababu za kiusalama, hatuwezi kusema," imesema kampuni hiyo kupitia taarifa iliyotoa.
Michael Obi, ambaye ana kampuni ya usafirishaji mjini Jos, hajaonekana tangu siku ya Ijumaa.
"Tunathibitisha kuwa Michael Obi ametekwa nyara, na kuwa waliomteka wamewasiliana na familia na wawakilishi wa familia na kuwa majadiliano ya kuachiliwa kwake yameanza," imesema taarifa hiyo.
Siku ya Jumanne, familia ya Obi ilipigiwa simu mara mbili na wateka nyara ambao walisema Michael amepelekwa Lagos.
Waliwasiliana na familia hiyo tena siku ya Jumatano ili kuwasilisha madai ya kikombozi, lakini polisi hawajasema kuhusu majadiliano zaidi yanayofanyika.

Comments