VILLA KUANZIA LIGI UGENINI

Villa Squad ya Dar es Salaam iliyopanda daraja msimu huu Agosti 20 mwaka huu itaanza michuano ya Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2011/2012 kwa kucheza ugenini dhidi ya Toto Africans kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza.
Mechi nyingine za raundi ya kwanza zitakuwa kati ya Coastal Union na Mtibwa Sugar (Mkwakwani, Tanga), Kagera Sugar na Ruvu Shooting (Kaitaba, Bukoba), Polisi Dodoma na African Lyon (Jamhuri, Dodoma) na Azam na Moro United (Chamazi, Dar es Salaam).
Raundi ya kwanza itamalizika Agosti 21 mwaka huu kwa mechi kati ya JKT Oljoro na Simba kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha na Yanga dhidi ya JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mzunguko wa kwanza (first leg) wa ligi hiyo utamalizika Novemba 5 mwaka huu wakati mzunguko wa pili (second leg) utamalizika Aprili Mosi mwakani ambapo jumla ya mechi 175 zitachezwa.
Pambano la watani wa jadi kati ya Yanga na Simba litafanyika Oktoba 29 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Mechi ya mzunguko wa pili ambapo Simba itakuwa mwenyeji itafanyika Aprili Mosi mwakani kwenye uwanja huo huo.


NGORONGORO HEROES YAALIKWA COSAFA
Timu ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 ya Tanzania (Ngorongoro Heroes) imealikwa kushiriki michuano ya umri huo ya Shirikisho la Vyama vya Mpira wa Miguu Kusini mwaka Afrika (COSAFA) itakayofanyika kuanzia Desemba 1-10 jijini Gaborone, Botswana.
Wachezaji wanaotakiwa kushiriki michuano hiyo ni wale waliozaliwa baada ya Januari 1, 1992. Timu zinatakiwa kuthibitisha ushiriki wao kufikia Agosti 17 mwaka huu na ratiba itapangwa Agosti 24 mwaka huu jijini Gaborone. COSAFA itachangia sehemu ya nauli ya timu shiriki kwenda kwenye mashindano hayo.
Ngorongoro Heroes inayofundishwa na Kim Poulsen akisaidiwa na Adolf Rishard hivi sasa inafanya mazoezi ya wiki moja kila mwezi.

Comments