STARS NA ALGERIA KIINGILIO BUKU TATU

Viingilio kwa ajili ya mechi ya mchujo kutafuta tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika mwakani nchini Equatorial Guinea na Gabon kati ya Taifa Stars na Algeria vitakuwa kama ifuatavyo; Viti vya kijani ni sh. 3,000, viti vya bluu sh. 5,000, viti vya rangi ya chungwa sh. 7,000, VIP C sh.10,000, VIP B sh. 20,000 na VIP A sh. 30,000. Tiketi zitaanza kuuzwa Septemba Mosi mwaka huu.
Taifa Stars tayari iko kambini tangu jana (Agosti 28 mwaka huu) na inaendelea na mazoezi Uwanja wa Karume ambapo wachezaji wote wa ndani waliripoti jana mchana na kuanza mazoezi jioni.
Wachezaji wan je waliofika jana usiku ni Abdi Kassim na Dan Mrwanda kutoka Vietnam na Mbwana Samata kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo. Athuman Machupa (Sweden), Henry Joseph (Norway) na Idrisa Rajab (Kenya) wanaingia leo jioni.
Nizar Khalfan wa Vancouver Whitecaps ya Canada ndiye atakayekuwa mchezaji wa mwisho kuripoti kambini. Khalfan atatua nchini kesho saa 5.15 usiku kwa ndege ya PrescisionAir akitokea Nairobi.

Comments