MREMBO WA SHINYANGA ATWAA TAJI LA MISS PHOTOGENIC

Mshindi wa taji la Miss Photogenic 2011, Tracy Sospeter akiwa katika poazi baada ya kutajwa kuwa ndie mshindi katika shindano hilo dogo katika shindano la Vodacom Miss Tanznia 2011 na kufanikiwa kuwa mrembo wa pili kuingia katika hatua ya 15 bora ya shindano hilo. Mshindi huyo alitangazwa akiwa mjini Arusha jana. (Picha na Mpigapicha wetu).

MSHIRIKI wa Vodacom Miss Tanzania Tracy Mabula(20) ameibuka mshindi wa taji la Vodacom Miss Photogenic baada ya kuwabwaga washiriki wengine 29 katika kinyang’anyiro hicho kilichofanyika mkoani Arusha ambapo warembo hao wapo kwa ziara ya mafunzo.
Kwa ushindi huo, mlimbwende tracy anayewakilisha mkoa wa Shinyanga, sasa atatumiwa na Vodacom Tanzania katika matangazo mbalimbali na tayari ameingia katika nafasi robo fainali .
Mkurugenzi wa Vodacom Tanzania kanda ya Kaskazini Nguvu Kamando amesema ushindi wa mrembo huo ni ishara kwamba ana muonekano unaoendana na utendaji wa kampuni hiyo unaofanya kazi kuendana na wakati uliopo.
“Mara nyingi tumekuwa tukitumia mawakala kututafutia watu wa kufanya matangazo ya bidhaa na kazi zetu mbalimbali, ni matumaini kipindi hiki Tracy atatuwakilisha vema katika kazi zetu na kuifikisha Vodacom inapotaka,” alisema Kamando.
Naye Mkurugenzi wa Lino Agency ambao ndio waandaaji wa Vodacom Miss Tanzania Hashim Lundenga alisema kitendo cha mshiriki huyo kuvikwa taji hilo ni kiashiria tosha kwamba shindano la Vodacom Miss Tanzania sio uhuni kama baadhi ya watu wanavyoliita.
“Baadhi ya watu wamekuwa wakiliita shindano letu kwamba linalokiuka maadili ya Kitanzania, kwa kitendo cha kampuni ya Vodacom kutuamini na kumchagua mmoja wa washiriki wetu kuwa balozi wao kinadhihirisha kazi yetu imelenga kuisaidia jamii katika kujiletea maendeleo,” alisema Lundenga.
Mbali na hayo Lundenga alimuomba mrembo huyo kuiwakilisha vema kamati ya Miss Tanzania huko aendako ili kutoa fursa kwa warembo wengine kuweza kutumiwa na kampuni hiyo jambo litakalowakomboa wanawake wa Kitanzania.
Kabla ya tracy kutangazwa mshindi, warembo wengine wane ambao waliingia fainali katika shindano hilo, ambao walitangazwa na Lundenga ni pamoja na Jeniffer Kakolaki,Christina William, Glory Lory na Zerulia Manoko.
“nimefurahi sana baada ya kushinda nafasi hii, na nina imani nitaitumia vizuri katika kutangaza kazi za Vodacom na nyingine ambazo ntapangiwa na kamati ya Miss Tanzania”alisema Tracy.
Kabla ya shindano hilo washiriki wa shindano hilo mwaka huu waliendelea na ziara hiyo kwenye Mikoa ya kanda ya Kaskazini na kupata fursa ya kutembelea kaburi la aliyewahi kuwa Waziri Mkuu Hayati Edward Moringe Sokoine.
Wakiwa eneo la Monduli warembo hao walipokelewa na Mtoto wa Sokoine Nameloki Sokoine ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum (CCM) mkoa wa Arusha aliyekuwa mgeni rasmi.
Akizungumzia ziara hiyo Meneja Uhusiano na Habari kwa Njia ya Mtandao wa Vodacom Tanzania Matina Nkurlu alisema washiriki hao wanajifunza vitu mbalimbali ikiwemo utalii wa ndani na rasilimali zilizopo nchini.
Mwaka huu warembo hao wameingia kambini kwa mfumo tofauti na uliozoeleka kwani wamewekwa kwenye jumba maalum la ‘Vodacom House’ ambapo matukio yao yatakuwa yakioneshwa kupitia Startv na Clouds TV na watazamaji watapata fursa ya kupiga kura kuchagua mrembo watakayemuona anafaa.

Comments