YANGA WALIPELEKA KOMBE LA KAGAME BUNGENI KESHO

MABINGWA  wa klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati  maarufu kama ‘Kagame Cup’ mwaka 2011, timu ya soka ya Yanga inatarajiwa kwenda mjini  Dodoma kesho kwa ajili ya kupeleka Kombe la Ubingwa kwa Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 Akizungumza jijini  Dar es Salaam jana mratibu wa ziara hiyo maalum Cellina Agustino, lengo la ziara hiyo ni pamoja na kuwapa nafasi wabunge hao kulishuhudia pamoja na wakazi wa mkoa wa Dodoma. 
Alisema, wachezaji wa Yanga  kesho watatinga katika bunge na kisha baadaye kujumuika na wabunge katika tafrija fupi waliyoandaliwa.


“Mara baada ya tafrija fupi, wachezaji wa Yanga jioni watafanya mazoezi yao kwenye Uwanja wa Jamhuri na keshokutwa Jumamosi watakuwa na mechi ya kirafiki dhidi ya timu ya Polisi Dodoma, “alisema .
 Alisema kupelekwa kwa kombe hilo bungeni ni ombi la Wabunge baada ya Tanzania kufanya vizuri katika mashindano hayo ikiwa ni pamoja kulibakisha kombe hilo Tanzania.
 Agustino alisema kuwa mechi hiyo ya kirafiki inawapa fursa wakazi wa Dodoma  na hasa mashabiki wa Yanga kuishudia timu hiyo ambayo pia ni bingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bar msimu wa 2010/2011. 
Alisema kuwa maandalizi ya kila kitu kimekamilika ambapo Yanga ittakuwepo mkoani humo kwa muda siku nne na kurejea Dar es Salaam siku ya Jumapili.

Comments