WASOMAJI MAGAZETI YA DIMBA, BINGWA KUONDOKA NA GARI

 Meneja Masoko na Usambazaji wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd, Grace Kassella, akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Promosheni ya Mchongo, inayoendeshwa na kampuni hiyo kwa kipindi cha miezi mitatu, ambako washiriki watajishindia zawadi mbalimbali, zikiwamo gari aina ya Toyota Vitz kwa upande wa magazeti ya michezo, Bingwa na Dimba na Toyota Suzuki kwa Gazeti la Mtanzania. Promosheni hiyo ilizinduliwa jana katika Ofisi za Kampuni hiyo, zilizopo Sinza Kijiweni, Dar es Salaam.

 Mratibu wa Promosheni ya Mchongo akionyesha sehemu zitakazopatikana kuponi kwenye gazeti la Mtanzania.
 Baadhi ya wafanyakazi wa Kampuni ya New Habari (2006) Ltd wakigawiwa mafaili yenye maelezo ya Kampuni.
 Hili ndilo gari aina ya Toyota Vitz, litakaloshindaniwa katika Promosheni ya Mchongo kwa upande wa magazeti ya Bingwa na Dimba, yanayochapishwa na Kampuni ya New Habari (2006) Ltd.
KAMPUNI ya  New Habari (2006) ambao ni watengenezaji wa magazeti ya Bingwa, Dimba, Mtanzania, Rai na The African, imezindua promesheni iliyopewa jina la Mchongo ambayo itampa msomaji wa magazeti yao matatu kujishindia zawadi ya gari na nyinginezo.
Akizungumza katika uzinduzi wa promosheni hiyo, Makao Makuu ya Kampuni hiyo, Sinza Kijiweni, jijini Dar es Salaam, Meneja Masoko na Usambazaji wa New Habari, Grace Kasella, alisema promosheni hiyo itawahusu wasomaji wa magazeti ya Bingwa, Dimba na Mtanzania.
Alisema kuwa wasomaji wa Bingwa na Dimba, watashindania gari dogo aina ya Vitz lenye thamani ya Sh milioni 8.5, wakati wale wa Mtanzania watawania gari aina ya Suzuki Vitara yenye thamani ya Sh milioni 14, katika droo kubwa itakayofanyika baada ya miezi mitatu, ikitarajiwa kumalizika Oktoba mwaka huu kwenye ofisi za kampuni hiyo.
“Zawadi hizo za magari pamoja na nyinginezo kama fulana, runinga, kofia, mipira na nyinginezo zitakazokuwa zikitolewa katika droo ndogo za kila mwezi, zina thamani ya Sh milioni 36,” alisema.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Usanifu Kurasa wa kampuni hiyo ambaye ndiye msimamizi wa promosheni hiyo, Essy Ogunde, alisema msomaji wa magazeti hayo, ataingia kwenye promosheni hiyo kwa kujaza kuponi inayopatikana kwenye magazeti hayo na kuituma katika ofisi za kampuni hiyo.
Alisema kuwa wafanyakazi wa kampuni hiyo pamoja na familia zao, hawataruhusiwa kushiriki na vigezo na masharti vitazingatiwa.

Comments