WAREMBO WA KANDA ZA KINONDONI, ILALA NA TEMEKE KUJIACHIA CLUB SUNCIRO KESHO

Kampuni ya Simu za Mkononi ya Vodacom Tanzania ambao ndiyo wadhamini wakuu wa Shindano la urembo la Vodacom Miss Tanzania linalotarajia kuanza hivi karibuni wameandaa usiku wa warembo utakaowahusisha warembo kutokakanda ya Kinondoni, Temeke na Ilala.
Tayari mchakato wa kuwapata warembo kutoka kanda hizo tatu umeshakamilika na kwamba Vodacom Tanzania imeeandaa usiku huo utakaofanyika Julai 8 mwaka huu kwenye Club Sun Sirro iliyopo Sinza jijini Dar es Salaam ili kuanza kuwaweka pamoja.
Afisa Udhamini  wa Vodacom Tanzania Ibrahim Kaude amesema kwa kuwa kunajitokeza kasoro za hapa na pale kabla na wakati wa kambi ya warembo hao kampuni yao imeona itumie fursa hiyo ili kuwandaa walimbwende hao kisaikolojia.
Akifafanua Kaude alisema kwamba mbali na hilo lengo lingine la Usiku huo wa Warembo ni kuanza kuhamasisha uwepo wa msimu huo wa Vodacom Miss Tanzania nchi nzima.
“Kama inavyoeleweka kuwa Vodacom Miss Tanzania ndiyo sindano kubwa la urembo nchini, hivyo ili kuondoa dhana kwamba kushiriki kwenye tukio hili ni uhuni tumewaandalia usiku wao ili wajifunze mambo mbalimbali ikiwemo kupata ujasiri na kuzoea hadhira,” alisema Kaude.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Miss Ilala Jackson Kalikumtima ameishukuru Vodacom Tanzania kwa kuandaa usiku huo ambapo amesema hiyo ni ishara kwamba shindano la mwaka huu litakuwa la kihistoria.
Vilevile Kalikumtima amefafanua kwamba, licha ya usiku huo kuwakutanisha pamoja warembo wa Ilala, Temeke na Kinondoni ambazo zina ushindani mkubwa pia utatoa changamoto kwa majaji na waandaaji wa kanda hizo kuhakikisha wanatoa walimbwende wenye vigezo.
Mbali ya usiku huo, Vodacom pia imekuwa na utaratibu wa kuwapeleka washiriki wa Vodacom Miss Tanzania kwenye maeneo mbalimbali ya kujifunza ikiwemo kwenye Hifadhi za Taifa, maeneo ya rasilimali na kufanya shughuli mbalimbali za kijamii.
Shindano la mwaka jana lililofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani City jijini lilimuibua Genevieve Mpangala kutoka Temeke kuwa ndiye mlimbwende wa 2010/2011 akivaa viatu vya Miriam Gerald aliyeuwakilisha mkoa wa Mwanza mwaka 2009.

Comments