TWIGA STARS KUFUNGUA NA GHANA ALL AFICA GAMES

Timu ya Taifa ya mpira wa miguu ya wanawake ya Tanzania (Twiga Stars) itaanza 
mashindano ya All Africa Games yatakayofanyika Septemba mwaka huu jijini Maputo, 
Msumbiji, Septemba 5 kwa kupambana na Ghana. 
Kwa mujibu wa ratiba ya michuano hiyo iliyotolewa jana Shirikisho la Mpira wa 
Miguu Afrika (CAF), Twiga Stars ambayo iko kundi B itacheza mechi ya pili 
Septemba 8 mwaka huu kwa kupambana na Afrika Kusini kabla ya kumaliza hatua ya 
makundi Septemba 11 mwaka huu dhidi ya Zimbabwe. 
Mechi za nusu fainali zitachezwa Septemba 13 na 14 mwaka huu wakati ile ya 
kutafuta mshindi wa tatu itakuwa Septemba 16 mwaka huu na fainali ni Septemba 17 
mwaka huu. Timu mbili za kwanza katika kila kundi ndizo zitakazofuzu kwa hatua 
ya nusu fainali. 
Kundi A katika michuano hiyo lina timu za wenyeji Msumbiji, Cameroon, Algeria na 
Guinea. Nigeria ndiyo waliokuwa mabingwa wa 2007, lakini hawakufanikiwa kufuzu 
kwa michuano hiyo mwaka huu ambayo hufanyika kila baada ya miaka minne.
 
Boniface Wambura 
Ofisa Habari

Comments