SHOGA YAMFANYA TINO AACHANE NA FILAMU ZA MALAVIDAVI

MSANII  maarufu wa filamu nchini,  Hissan Muya ‘Tino’, (pichani) ameapa kutocheza tena filamu za kimapenzi badala yake atacheza filamu za mapigano zinazoelimisha jamii.
Akizungumza hivi karibuni Tino alisema kuwa kwa sasa amesitisha mpango wa kutengeneza na kucheza  filamu za mapenzi kwa kuwa wengi wamejikita kutengeneza filamu za aina hiyo na kusahau mambo muhimu yanayoigusa jamii hasa janga kubwa la ukimwi, njaa na mengine mengi.
Tino alisema sababu nyingine ya kuzitosa filamu za mapenzi ni baada ya kutengeneza filamu  ya ‘Shoga’ na baadaye kubadilishwa jina na kuitwa ‘Shoga yangu’  iliyokuwa na lengo la kuelimisha jamii kuhusu suala zima la ushoga, badala yake ijana kumletea matatizo.
“Sitaki kucheza tena filamu za mapenzi, sasa hivi nataka kugeukia kwenye filamu za mapigano na zile zinazogusa maisha ya binadamu wa kawaida,” alisema Tino.
Tino ambaye kwa sasa anatesa na filamu yake mpya ya ‘Shoga yangu’ ambayo ipo sokoni, amewashauri wasanii wengine kutojikita sana katika filamu za mapenzi, ambapo alisema kuna stori nyingi zikiwemo zile za Watanzania wanaopatwa na majanga mbalimbali hapa nchini.

Comments