RT YAHIMIZA MIKOA KUTHIBITISHA KUSHIRIKI MASHINDANO YA TAIFA

CHAMA cha riadha Tanzania (RT), kimeitaka mikoa kuthibitisha mapema kushiriki kwenye mashindano ya Taifa yanayotarajia kufanyika Julai 23 hadi 24 kwenye Uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam. 
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana Katibu Mkuu wa RT, Mujaya Suleiman Nyambui alisema kuwa kwa mikoa inayotaka kushiriki inatakiwa kufanya hivyo kuanzia Julai 15 hadi 20 mwaka huu. 
Alisema kuwa mikoa mipya ambayo haijawahi kushiriki mashindano hayo inatakiwa kutoa taarifa mapema ili waweze kujua idadi kamili ya mikoa itakayoshiriki mwaka huu. 
“Tunaiomba mikoa mipya itujulishe mapema ili tuweze kufanya maandalizi ya sehemu za kufikia pamoja na chakula wakati wa kufanyika kwa mashindano watupe na idadi kamili ya wachezaji wao” alisema Nyambui. 
Alisema tayari walishaitumia barua za mialiko mikoa hiyo kwa ajili ya kushiriki mashindano hayo yenye lengo la kusheherekea madhimisho ya miaka 50 ya uhuru wa Tanzania ambapo hushirikisha mikoa yote. 
Mashindano hayo hufanyika kila mwaka ambapo mwaka jana yalishirikisha mikoa zaidi ya 20 ambapo yalifanyika katika Uwanja wa taifa Jijini Dar es Salaam.

Comments