BASATA: TUZO NI KUTHAMINI MCHANGO WA WASANII

Msanii wa kizazi kipya Khamis Ramadhan aka H-Baba (Katikati) akiwasilisha mada kwenye Jukwaa la Sanaa linalofanyika kila wiki Kwenye Ukumbi wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA).Kulia kwake ni Afisa wa Sanaa kutoka BASATA Bw.Lawrance Hinju na Kaimu Mratibu wa Jukwaa hilo Agnes Kimwaga.
Mkongwe wa muziki wa dansi nchini Kassim Mapili akimpa ushauri msanii H-Baba mara baada ya kumaliza kuwasilisha mada yake kwenye Jukwaa la Sanaa wiki hii.
Mdau wa Jukwaa la Sanaa akimuuliza masuala mbalimbali Msanii H-Baba
Wadau wakifuatilia kwa makini mada kwenye Jukwaa la Sanaa.


Na Mwandishi Wetu


Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limesema kwamba,tunzo mbalimbali zinazotolewa kwa wasanii zinalenga kuthamini mchango wao katika tasnia na kujenga hali ya ushindani miongoni mwao katika kubuni kazi zilizo bora.


Hayo yamesemwa na Afisa wa Sanaa wa Baraza hilo,Bw.Lawrance Hinju wakati akiliahirisha Jukwaa la Sanaa linalofanyika kila Jumatatu makao makuu ya BASATA eneo la Ilala Sharif Shamba,Dar es Salaam.


Alisema kwamba,tunzo kama zile za muziki zimekuwa zikitolewa miongoni mwa wasanii kwa kuzingatia vigezo mbalimbali vya kitaaluma ambavyo mara kwa mara vimekuwa vikitangazwa na Baraza katika kuhakikisha kweli wale wanaoshinda ndiyo wanaokuwa wanastahili na wenye kazi bora.


“BASATA imebuni tuzo za muziki kwa lengo la kuthamini mchango wa wasanii na kujenga ushindani miongoni mwao.Tuzo inaweza ikawa cheti au kitu chochote lakini Baraza kwa kushirikiana na mwendeshaji limeona liwe linatoa tuzo hizo maalum inayoambatana na fedha taslimu” alisema Bw.Hinju.


Aliongeza kwamba,kulingana na idadi ya maeneo yanayoshindaniwa si rahisi kwa wasanii wote kupata ingawa kuna kila sababu ya wao (wasanii) kujikita katika kutengeneza kazi zenye ubora, zenye maadili ndani yake na zilizo na uhalisia ndani ya jamii ili mchango wao uonekane na kutuzwa.


Awali akiwasilisha mada kwenye Jukwaa la Sanaa kuhusu Umuhimu wa Kubuni Vitu vipya kwenye Muziki wa kizazi kipya,Msanii Khamis Ramadhan aka H-Baba alisema kwamba,wasanii wa kizazi kipya wanatakiwa kubadilika na kupendana kwani kumekuwa na tatizo sugu la kuhujumiana na kufitiniana miongoni mwao.


“Nasema wazi kabisa wasanii hatupendani,tunatakiwa kubadilika ili kuweza kupata mafanikio.Haiwezekani kufika kokote kwa hali hii” alilalamika H-Baba.

Jukwaa la Sanaa linalofanyika kila Jumatatu kwenye Ukumbi wa BASATA limekuwa ni eneo huru kwa wasanii, waandishi wa habari na wadau wa sanaa kuelimishana na kupashana habari kuhusu mambo mbalimbali yahusuyo tasnia hiyo.

Comments