KUMEKUCHA HAYE NA KLITSCHKO

Wladimir Klitschko (KUSHOTO) na David Haye katika mkutano na Waandishi wa Habari Juni 27, 2011 mjini Hamburg, Ujerumani
HII ni sawa na mwisho wa dunia, kwani pambano kati ya mabondia wawili wenye nguvu na uwezo mkubwa jukwaani, wanakutana Jumamosi, katika pambano ambalo linasubiriwa kwa hamu kubwa na watu wengi.
Wanaokutana si wengine isipokuwa ni mtu mwenye ngumi za kuua, Klitschko Wladimir Klitschko atakayepanda ulingoni kujaribu kumtwanga David Haye.
Pambano hilo linatarajiwa kufanyika nchini hapa, huku likishirikisha mabondia kutoka nchi mbili tofauti zenye mawazo na uelewa tofauti wa kupigiana kampeni.
Klitschko anatoka Ukraine wakati Haye yeye ni mtoto wa London. Tayari vyombo vya habari vya Uingereza ambavyo vinafahamu fika nini maana ya upambe, vimeanza kufanya kazi yake.
Habari kubwa kwao kwa sasa ni chochote kile kinachosema na Haye, huku Klitschko akiwa anamalizwa kabla hata hajapanda kwenye jukwaa. Hapa ndipo utakapojua nini maana ya vyombo vya habari vya Uingereza, pale vinapoamua kumshabikia mtu wao.
Juzi, Haye katika mkutano na waandishi wa habari alivaa fulana inayomuonyesha anamchakaza kwa kiwango cha mauaji Klitschko, huku kukiwa na picha nyingine akionyeshwa kabebwa katika gari la wagonjwa.
Klitschko amekuja juu na kudai huo si uungwana kwani hilo ni pambano tu, hivyo kudhihirisha kuna mtu ataenda kufa ni sawa na kuwafanya watu wengine waogope.
Lakini pamoja na Klitschko kulalamika, Haye amesisitiza na kusema atafanya kile alichoonyesha kwani nia yake kubwa ni kummaliza kwa kiwango kikubwa na cha mauaji mpinzani wake huyo.
“Aache kulalamika, huu ni ukweli naenda kufanya kile ambacho dunia itakishangaa, kwani nataka kummaliza mapema, tena mapema zaidi.
“Ninataka kumuangamiza mapema mno na ninataka kufanya kile ambacho dunia itaamini,” alisema.
Kaka wa Klitschko, Vitali, amemtaka Haye kusema maneno hayo siku inayofuata mara baada ya pambano tena katika vyombo vya habari vya Uingereza ili sura yake iweze kuonekana vizuri kwa kile atakachokuwa amefanywa.
“Acha mkwara, mara baada ya kummaliza ndugu yako nitakusaka wewe. Usiende hospitali pamoja naye, ila cha msingi fahamu unakuja na gari la wagonjwa.
David Haye tayari ametoa mpaka nyimbo inayoitwa 'David Haye's Knockout', ambayo inasikika kwa watumiaji wa simu katika nchi kadhaa za Ulaya.
Klitschko anaonekana mkimya zaidi na kutotaka kusema mengi, lakini Haye ana mdomo mno na ametamka pia mpinzani wake huyo ni sawa na mashine na atahakikisha anaiharibu katika pambano lao hilo la uzito wa juu kuwania taji la dunia.
Haye, 30, ambaye ana mkanda unaotambuliwa na WBA atakwaana na Klitschko, mwenye mkanda unaotambuliwa na IBF na WBO katika pambano hilo litakalofanyika katiuka mji wa Hamburg.
“Klitschko ni sawa na robot, sasa mimi nataka niwaambie watu waje kushuhudia jinsi ambavyo inavyoharibiwa na haitaweza kusimama tena.
Haye alitakiwa kukwaana na Klitschko mwaka 2009, lakini pambano hilo likaahirishwa kutokana na kuumia.
“Nashukuru kwamba pambano hili halikufanyika kipindi hicho, kwani kwa sasa niko safi zaidi kuliko kipindi kingine chochote kile.
“Hapa niko safi na nitaondoka jukwaani nikiwa bora zaidi, ila hii sura ya Klitschko ni lazima iende kukarabatiwa mara baada ya pambano hilo.”
Kaka wa Klitschko, ambaye naye ni bondia ameapa pia kwamba mara baada ya mdogo wake kumshughulikia Haye atahakikisha anafanya kila mbinu ili watwangane ili ammalize kabisa.
“Hizi nyodo zako zitakwisha tu. Subiri uone kitakachukutokea, maana umeingia katika anga ambazo hazikufai,” alisema Vitali.
Haye mpaka sasa amepambana mapambano 28, ambapo katika hayo ameshinda 25 ambapo 23 ni kwa knockout, huku akipigwa pambano moja.
Klitschko amepigana mapambano 58 ambapo ameshinda mapambano 55, ambapo 49 ni kwa knockout, huku akipigwa mapambano matatu.
Nani kuondoka mbabe? Ni kitu cha kusubiri na kuona.

Comments