KINYWAJI CHA CASTLE LAGER KUDHAMINI MICHUANO YA KAGAME

KAMPUNI ya bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chake cha Castle Lager inatarajia kutumia zaidi ya shilingi mil.300 kama sehemu ya udhamini wao wa michuano ya klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati maarufu kama 'Kagame castle Cup' inayotarajiwa kuanza juni 25 hadi julai 9 jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, mkurugenzi wa masoko wa TBL, David Minja alisema kampuni yao inawajibika kudhamini michuano hiyo mikubwa katika ukanda huo kwa lengo la kukuza na kuendeleza vipaji.
Alisema kupitia udhamini huo wamejikita katika kusaidia malazi, usafiri wa ndani na matangazo katika vyombo vya habari ili kusaidia kuleta msisimko wa michuano sambamba na kuwaweka watu karibu katika kufuatilia michuano hiyo.
"Udhamini wetu pia utatoa mchango mkubwa kuhakikisha kiwango cha soka Afrika Mashariki na KAti kinakua katika ngazi ya vilabu na timu za taifa ili matraifa yetu yaweze kufuzu kushiriki kombe la dunia mwaka 2014,"Alisema Minja.
Kwa upande wake Rais wa baraza la vyama vya soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Leodger Tenga aliishukuru TBL kwa kudhamini michuano hiyo na kusema kuwa kujitosa kwao kutasaidia kuongeza kiwango cha soka katika ukanda huo.
"Baada ya Sudan kushindwa kuendesha michuano hiii na Cecafa kutuipa jukumu hilo, tuliamua kuwafuata ninyi...ingawa kwa muda mfupi tu lakini mmeweza kukubali kudhamini michuano hii hali inayoonyesha mnaunga jitihada za kusaka mafanikio9 katika soka, tunawashukuru sana.
Aidha,Tenga alivitaka vilabu vitakavyoshiriki michuano hiyo kuonyesha ushindani mkubwa ili bingwa apatikane kihalali."Kama raisi wa Cecafa nitafurahi timu nzuri ikishinda, na kama raisi wa TFF (Shirikisho la Soka Tanzania) nitafurahi kuona moja ya timu za hapa nchini inashinda", Alisema Tenga.
Naye Katibu mkuu wa Cecafa Nicolaus Musonye, pamoja na kuishukuru TBl kwa kudhamini michuano hiyo alisema, mdhamini mwingine kutoka nchini Sudan amejitokeza kugharamia tiketi za ndege kwa timu zote zitakazoshiriki, huku dola 60,000 kwa ajili ya zawadi za washindi kama kawaida zitatoka kwa rais wa Rwanda, Paul Kagame.
Alisema timu 12 zinazotarajiwa kushirikimichuano hiyo itakayopigwa katika vituo vitatu zinatarajiwa kuanza kuwasili nchini kuanzia kesho, huku ratiba ya michuano hiyo inatarajiwa kutolewa leo.
Timu zilizothibitisha kushiriki ni pamoja na Yanga,Simba (Tanzania), Ulinzi (Kenya), St.George (Ethiopia), El Mareikh (Sudan), Ocean View (Zanzibar), Banambwaya (Uganda), Red Sea (Eritrea), Elman (Somalia), Port FC (Djibout), Vitalo (Burundi), Eticele na mabingwa watetezi, APR zote kutoka Rwanda.

Comments