TFF YAANDAA KOZI YA UKOCHA PEVU

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupitia Kurugenzi ya Ufundi limeandaa kozi ya ukocha ngazi pevu (advanced level) itakayofanyika Dar es Salaam kuanzia Juni 6-19 mwaka huu.
Wakufunzi wa kozi hiyo itakayoshirikisha makocha 24 kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara watakuwa Sunday Kayuni, Jan Poulsen na Salum Madadi. Ada ya kushiriki ambayo italipwa TFF kabla ya kuanza kozi ni sh. 50,000 ambapo washiriki wanatakiwa kuthibitisha ushiriki wao kwa maandishi kabla ya Juni Mosi.
Washiriki watajitegemea kwa nauli ya kuja na kurudi, chakula, malazi na vifaa vya mazoezi. TFF itatoa chai na chakula cha mchana kwa kipindi chote cha kozi hiyo.
Makocha walioteuliwa kushiriki ni Abdul Nyumba, Abubakar Balingula, Bakari Shime, Dady John, Emmanuel Makoye, Emmanuel Massawe, Fulgence Novatus, Ibrahim Mulumba, Juma Mgunda, Jumanne Mtambi, Leonard Jima, Leonard Barongo, Leticia Muganga, Lister Manyala, Maka Mwalwisi, Makoye Mayige, Nicholas Achimpota, Oswald Mchopa, Peter Mhina, Salvatory Buchweishaja, Tiba Mlesa, Venance Kazungu, Victoria Chiefundo na Vitalis Salila.

COPA COCA COLA 2011 NGAZI YA TAIFA
Michuano ya Copa Coca Cola ngazi ya Taifa itaanza Juni 11 mwaka huu kama ilivyopangwa ambapo timu zinatakiwa kuwasili Kibaha mkoani Pwani (Shule ya Sekondari Filbert Bayi0 kuanzia Juni 6 mwaka huu.
Awali tulipendekeza michuano ya ngazi ya Taifa ifanyike katika vituo vya Arusha, Dar es Salaam na Mwanza, na baadaye fainali jijini Dar es Salaam. Mapendekezo hayo hayakuwezekana, hivyo ngazi hiyo itafanyika Kibaha na Dar es Salaam.
Baada ya hatua ya makundi, kutakuwa na hatua ya mtoano ya 16 bora ili kupata timu nane zitakazoingia robo fainali.

Boniface Wambura
Ofisa Habari TFF

Comments