MISS MWANZA 2011 KUZINDULIWA JUNI MOSI

UZINDUZI wa shindano la urembo kumsaka Miss Mwanza 2011, unatarajiwa kufanyika 
Juni Mosi, mwaka huu kwenye ukumbi wa Hoteli ya Kitalii ya Gold Crest iliyopo 
katika jengo la PPF, katikati ya Jiji la Mwanza.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Kampuni ya Sisi Entertainment, waandaaji wa shindano 
hilo, John Dotto, uzinduzi huo utaambatana na utambulisho wa warembo 
watakaochuana katika kinyang’anyiro hicho.
Alisema kuwa tayari warembo wameshaanza kujiandikisha kuwania Umalkia wa Mwanza 
na kwamba wanaojiona kuwa na sifa za kushiriki mashindano hayo, wanakaribishwa 
ambapo fomu zinapatikana katika ofisi za hoteli hiyo.
“Bado tunakaribisha warembo wenye sifa kujiandikisha kwa sasa kwani baada ya 
uzinduzi, hatutapokea mrembo yeyote yule, hata awe na sifa kiasi gani,” alisema.
Alisema kuwa shindano lao linatarajiwa kuwa la kiwango cha juu, kuanzia 
maandalizi yake, warembo na shoo ya kilele cha kinyang’anyiro hicho.
Dotto alisema kwamba lengo lao mwaka huu ni kumtoa Miss Tanzania kama ilivyokuwa 
miaka ya 2008 na 2009, wakiamini hilo linawezekana kutokana na jinsi 
walivyojipanga.
Warembo waliotokea Mwanza na kutwaa taji la Miss Tanzania na miaka yao katika 
mabano, ni Nasreen Karim (2008) na Miriam Gerald (2009) ambao walikatisha 
kutamba kwa Jiji la Dar es Salaam katika mashindano hayo kutokana na kutwaa taji 
la Miss Tanzania mara nyingi zaidi.
Dotto alisema: “Wadhamini wanaendelea kujitokeza na kwamba hadi sasa tunao PSI, 
Vodacom Tanzania na Redd’s, wengine wanakaribishwa kujitokeza kudhamini shindano 
hilo lenye historia ya kutoa Mrembo wa Taifa kwa miaka mwili mfululizo, 2008 na 
2009.”

Comments