KWA HILI LA GONGO LA MBOTO YANGA WAMEJIDHALILISHA!


WIKI iliyopita msafara wa wachezaji na viongozi kadhaa wa klabu ya Yanga, ulifanya ziara kwa baadhi ya wananchi walioathiriwa na milipuko ya mabomu iliyotokea eneo la Gongo la Mboto, jijini Dar es Salaa usiku wa Februari 16.
Hilo ni tukio unaloweza kuliita ajali baada ya mabomu hayo kuanza kulipuka katika Ghala Kuu lililopo katika Kambi ya 511 KJ, ambapo watu wapatao 24 walifariki dunia na zaidi ya 300 kujeruhiwa.
Zaidi ya hapo, ajali hiyo imeacha adha kubwa kwa wakati wa maeoneo hayo kwa wengine kukosa makazi kutokana na nyumba zao kubaki vifusi na nyingine zikipata madhara.
Siku chache baada ya milipuko ile, wachezaji wa Yanga ndipo walifanya ziara ya kuwajulia hali wananchi waliopatwa na athari mbalimbali kama si kufiwa na ndugu na jamaa zao, basi waliopoteza makazi yao.
Naomba niweke wazi kabla sijafika mbali katika Mtazamo wangu huu kwamba, hatua ya wachezaji wale kwenda kuwatembelea wananchi wale waliopo kwenye majonzi na simanzi, ni kitu cha kupongezwa na kuigwa.
Kutokana na kuguswa na hatua ile ya Yanga, baada ya kupata taarifa kuwa wachezaji na baadhi ya viongozi wangekwenda Gongo la Mboto, nilipata shauku ya kuambatana nao kwa manaa ya kwenda kuripoti tukio hilo la kuigwa.
Siku iliyofuata, mimi na baadhi ya waandishi tukaenda eneo husika kwa lengo la kuchukua taarifa, ingawa awali kulikuwa na taarifa kuwa kungekuwa na usafiri kwa waandishi ambao ungeanzia makao makuu ya klabu hiyo, makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani, Kariakoo jijiji Dar es Salaam.
Baada ya kuona usafiri huo unakawia, tuliamua kutangulia kwa lengo la kwenda kuripoti kile kinachotokea pia kama sehemu ya Watanzania kujionea kiwango cha athari zilizowapata wenzetu.
Tukiwa njiani, tlikuwa tukiwasiliana na viongozi wa Yanga ambao walitutaarifu timu inakuja, tulifika mida ya saa sita na kuendelea na mambo mengi huku tukisubiri ujio wa wachezaji wa Yanga.
Hatimaye wachezaji hao walifika majira ya saa nane mchana na kushusha walichokuja nacho na kukaa kando kusubiria ambapo muda ule alikuwepo Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha.
Kimsingi nakubaliana na usemi kuwa, kutoa ni moyo wala si utajiri na Mwenyezi Mungu huweza kumbariki hata aliyetoa kidogo cha msingi tu awe amekitoa kwa moyo mkunjufu.
Hata hivyo kile kilichotolewa siku ile na wachezaji wa Yanga na viongozi wao kadhaa akiwemo Mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Mohammed Bhinda, ni kuidhalilisha klabu hiyo kuanzia viongozi hadi wanachama wake.
Nasema hivi kutokana na kile kilichotolewa na wachezaji wa timu hiyo hakiendani hata kidogo na umaarufu na hadhi ya Yanga.
Inagawa cha bure hakina nyongeza, lakini wachezaji wa Yanga na viongozi wao, si wa kutoa katoni 10, sabuni na kalamu, vyote vikiwa na thamani kama ya sh 70,000.
Tuliambiwa kuwa wachezaji hao walichangishana fedha na kununua vitu, ni jambo zuri , lakini kwa upande mwingine haiingii akilini kwa timu kubwa kama ile kupeleka msaaada kama ule.
Hata baadhi ya wananchi waliokuwa pale waliuponda msaada ule na kudai haikustahili kuchoma mafuta ya gari na kupoteza muda wao kwenda kule, sana wangeamugiza hata dereva tu kuwawakilishia.
Kwa timu kubwa kama Yanga, umaarufy walionao wengi wa wachezaji haikupaswa kwwenda kutoa msaada wa kiwango kile na hasa ikizingatiwa uwezo walionao wachezaji hao inagwa si mkubwa sana.
Kwa mshahara, pamoja na posho wanazolipwa wachezaji wa Yanga hata kama wangechangishana hata sh.5,000 kila mchezaji nadhani wangepata kiasi cha fedha na kupeleka vitu vya maana kuliko walivyopeleka.
Hata uongozi nao unaonyesha ni jinsi gani haukuwa makini katika hilo kwani hata wajumbe wa kamati ya utendaji walioambatana na wachezaji hao Tito Ossoro, Bhinda na Katibu Celestine Mwesigwa walichukulia ni jambo la kawaida.
Ndio maana waandishi wa habari walipohoji udogo wa thamani ya vitu hivyo, waliambulia kejeli kwamba hata kama ni shilingi moja, yatosha kwa sababu ni msaaada tu.
Hivi kweli viongozi waliomakini wanaweza kuruhusu mambo ya aibu kama hayo?
Cha kushangaza ni kwamba, ziara ya Gongo la Mboto haikuwa ghafla, ilijulikana siku moja kabla, hivyo walipaswa kufanya maandalizi ya kutosha hata ya kuchangishana walau wapate cha kununua.
Siwezi kuwalaumu sana wachezaji wa Yanga kwani wale ni kama watoto, walipaswa kusimamiwa kwa maana ya kupewa mwongozo wa nini kifanyike, lakini kwa uzembe wa viongozi, aibu inaangukiwa kwa Yanga nzima.
Mimi nadhani, umefikia wakati viongozi kujua nini wanachokifanya, naamini wangejitambua wasingekubali
aibu kama ile ambayo imeitia doa klabu nzima badala ya kuimwagia sifa.
Na huu ndio Mtazamo wangu, washkaji msijenge chuki!
www.mamapipiro.blogspot.com, mamapipiro@yahoo.com, 0788 344 566.

Comments

  1. Dada unaipenda Simba vibaya. Wewe mwenyewe umejichanganya toka mwanzo, umesema ni msaada, halafu ukasema kutoa ni moyo...sioni argumentative yeyote kwenye makala yako hii zaidi ya mapenzi binafsi. Sasa hata kama wangetoa 1 million then ungesema pia ni ndogo kulingana na jina la timu yenyewe.

    ReplyDelete
  2. Hivi AZAM na VILLA SQUAD WAMETOA TANI NGAPI ZA ZA MIHOGO HUKO GOMZ?MASELA MSIJENGE CHUKI NATAKA TU KUPATA TAARIFA KWA KUWA NIKO MBALI NA TUKIO

    ReplyDelete
  3. kungwi la kimanyemaMarch 1, 2011 at 5:23 PM

    Acha utoto bi dada,inaonekana hapo hasira ni kunyimwa usafiri wa kwenda gongo la mboto,kwani na nyie na genge lenu hamkuguswa?hebu tuelezeni wenzetu mlitoa katoni ngapi kutokana na ukongwe wenu kwenye fani

    ReplyDelete
  4. Swali: Wangeenda mikono mitupu kabisa ingekuwaje? Kweli utamaduni wetu wa kutothamini vitu na kutanguliza ubinadamu sasa umekwisha. Sasa usipopeleka zawadi/kifutajasho kikubwa unaonekana hufai. Mashindano haya hayaishii hapa. Ndiyo maana tunashindana kuwa na maharusi makubwa na ya gharama kubwa kupindukia ili tu kumzidi fulani. Ndiyo maana tunapambana kununua magari ya bei mbaya ili kumzidi jirani. Ndiyo maana hata wakubwa wetu nao wanashindana kufisadika. Mashindano haya ya vitu yanatupeleka wapi kama jamii?

    Hongereni wachezaji na viongozi wa Yanga kwa kuacha shughuli zenu muhimu na kwenda kuwajulia hali ndugu zenu wa Gongo la Mboto. Kwangu mimi hata kama mngeenda mikono mitupu nisingewalaumu. Hamstahili lawama hata kidogo na Mola ameshauona wema wenu !!!

    ReplyDelete
  5. Hawa ni Simba sana, hii ni hasira ya kukosa usafiri na vinywaji, wanapenda kula bure sana hawa.

    ReplyDelete
  6. HIVI AZAM NA JKT RUVU WAMETOA TANI NGAPI?

    ReplyDelete
  7. Kutoa ni moyo chochote pokea

    ReplyDelete

Post a Comment