SMG, MACHUPA, SHIBOLI WAITWA TAIFA STARS

SAID MAULID
WACHEZAJI kadhaa wanaocheza soka la kulipwa akiwemo Said Maulid 'SMG' na Athuman Machuppa wameitwa katika timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ ambayo itaingia kambini Desemba 27 kujiandaa na mashindano ya ‘Nile Basin’ nchini Misri.
Kocha msaidizi wa timu hiyo Sylvestre Marsh ametangaza kikosi hicho jijini Mwanza akimwakilisha Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mdenish Jan Poulsen, ambaye yuko likizo nchini kwao Denmark.
Marsh amewataja ‘SMG’ anayekipiga Marquis de Angola, Athuman Machupa anayekipiga nchini Sweden.
Pia yumo nyota mpya wa klabu ya Simba, Ally Ahmed Shiboli, na Geofrey Taita wa Kagera huku pia mshambuliaji wa Yanga, Jerry Tegete akirudishwa kundini na Mohammed Banka akitemwa.
Nyota wengine walioitwa ni makipa Juma Kaseja, Shabani Kado na Mohammed Said.
Walinzi ni Shadrack Nsajigwa ‘Fusso’, Stephano Mwasika, Aggrey Morris, Kelvin Yondani, Juma Nyoso na Nadir Haroub ‘Cannavaro’.
Viungo yupo Idrisa Rashid, Nurdin Bakari, Shabani Nditi, Henry Joseph, Jabir Aziz na Abdi Kassim ‘Babi’.
Washambuliaji wako Salum Machaku, Mrisho Ngasa na Nizar Khalfan.
Mashindano hayo yanashirikisha nchi za ukanda wa Ziwa Victoria na Mto Nile ambazo ni pamoja wenyeji Misri, Kenya, Uganda, Sudan na Tanzania ambayo imepangwa kutupa karata yake ya kwanza Januari 5 mwakani kwa kuvaana wa ‘Mafarao’ hao.

Comments