WADAU WALIA NA COSOTA, WATAKA IWE CHINI YA BASATA

Dkt.Aldin K. Mutembei ambaye ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Taaluma za Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (TATAKI) akichangia mada.Alitaka elimu zaidi itolewe kwa wasanii juu ya sheria za hakimiliki ikiwa ni pamoja na Cosota kuwa na sheria zenye kukidhi matakwa.
Mkurugenzi wa Rulu Arts Promotion,Ruyembe C.Mulimba akizungumzia utafiti uliofanywa na asasi yake juu ya mianya inayosababisha sheria ya hakimiliki chini ya Cosota kupwaya na kushindwa kuwapa wasanii stahiki zao.

Na Mwandishi Wetu,Mwanza
Wajumbe wa kikao cha nane cha sekta ya utamaduni kinachoendelea jijini Mwanza katika Ukumbi wa Benki Kuu maeneo ya Kapripoint wamelia na utendaji wa Chama cha Hakimiliki (Cosota) huku wakitaka kitengo kinachohusika na haki za wasanii kiwekwe chini ya Wizara ya Habari,Vijana, Utamaduni na Michezo hasa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA).
Wakichangia mada ya Utamaduni Kama Ajira na Maendeleo kwa Taifa iliyowasilishwa na Mtaalam wa Wizara ya Viwanda na Biashara Bw.Aristides Mbwasi,wajumbe wengi waliochangia walisema kwamba, hawaoni mantiki ya Chama cha hakimiliki za wasanii kuwa chini ya wizara ya Viwanda na Biashara wakati wasanii wenyewe wako wizara tofauti.
“Ndugu Mwenyekiti wa kikao hiki,Cosota inayotakiwa kulinda haki za wasanii iko chini ya watendaji wa wizara tofauti na ya wasanii,mbaya zaidi watendaji wake hawana utaalamu wala uzoefu katika tasnia ya sanaa.Nadhani sasa ni muda muafaka wa mamlaka hii inayolinda haki za wasanii na kazi zao iwe chini ya BASATA ambayo ndiyo inayolea wasanii na wadau wa sanaa” alichangia Bw.Mbogo,Afisa Utamaduni wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma huku akitaka Cosota ibaki na kulinda hamimiliki ya masuala mengine ikiwa chini ya wizara hiyohiyo.
Aliongeza kwamba, kumekuwa na lawama nyingi dhidi ya Cosota katika kulinda haki na kazi za wasanii na hili limekuwa likitokana na kushindwa kuonesha meno yake hasa kwa kubana vyombo vya habari ili vilipe mirahaba kwa wasanii na zaidi watendaji wa mamlaka hiyo kutokuwa na uelewa wa tasnia ya sanaa na wasanii wenyewe.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa RULU Arts Promotion,Ruyembe Mulimba alisema kwamba, asasi yake ilifanya utafiti katika nchi mbalimbali duniani ili kubaini mianya inayosababisha kupotea kwa haki za wasanii nchini na kuja na mapendekezo mbalimbali lakini ni bahati mbaya kwamba pamoja na kuyawasilisha Cosota hadi leo hayajafanyiwa kazi.
“Utafiti ulifanyika katika mataifa mengi yaliyofanikiwa katika eneo hili la hakimiliki kwa wasanii na mapendekezo yalipelekwa Cosota kukatolewa ahadi kwamba yangefanyiwa kazi ifikapo Desemba mwaka jana lakini hadi leo hakuna kilichofanyika na makabrasha haieleweki yanafanyiwa nini” alihoji Ruyembe.
Aliongeza kwamba, ni vema Cosota wakafanyia kazi mapendekeo hayo ya utafiti kwani yameshirikisha wataalam mbalimbali wa sekta ya sanaa, viwanda na biashara wakiwemo Cosota wenyewe hivyo njia pekee ya kulinda haki za wasanii na kazi zao ni kubadili sheria zilizopo ili ziwe na meno na kuweza kuwapatia wasanii stahiki zao.
Kwa muda mrefu kumekuwa na malalamiko ya wadau wa sanaa dhidi ya wizi wa kazi zao hali ambayo inatajwa kusababisha ufukara miongoni mwao.

Comments