WASANII WA KIUME WANAWADHALILISHA WENZAO WA KIKE

Rais wa Bendi ya FM Academia ‘Wazee wa Ngwasuma’ Nyoshi El Saadat(aliyevaa tisheti ya rangi ya orange) akichangia mada kwenye Jukwaa la Sanaa.Alisema kwamba,muziki wa dansi umekua lakini wanamuziki hawafaidiki na kazi zao.Wengine kutoka kushoto ni Katibu Mtendaji BASATA,Bw.Materego,Luiza Mbutu na Hassan Bumbuli Katibu wa CAJAtz.

 


Wasanii wa kiume hususan wa muziki wa dansi ikiwa ni pamoja na wapenzi wa
muziki huo wametajwa kuwa chanzo cha kuwadhalilisha wasanii wa kike hali
ambayo imekuwa ikisababisha waonekane chini pia wasio na maadili ndani ya
jamii.
Akizungumza kwenye Jukwaa la Sanaa Jumatatu hii,Muimbaji mahili wa Bendi
ya African Stars ‘Twanga Pepeta’,Luiza Mbutu alisema kwamba hali imekuwa
mbaya kiasi kwamba wasanii wa kike hususan wanenguaji wamejikuta wakifanya
mambo kinyume cha maadili ili kukidhi matakwa ya wasanii wa kiume na
baadhi ya wapenzi wa muziki wa dansi.
Akitoa mfano wa udhalilishaji huo, Luiza Mbutu alizungumzia tabia chafu ya
(wapenzi wa muziki wa dansi) ‘mapedeshee’ kuwatuza fedha wanenguaji wa
kike wawapo kwenye maonyesho kwa kuwawekea fedha kwenye matiti yao au
makalio hali ambayo imekuwa ni ya kidhalilishaji kwa kiwango cha juu.
“Wanenguaji wa kiume wamekuwa wakituzwa fedha kwa kupewa mikononi au
mifukoni lakini wale wa kike wamekuwa wakiwekewa kwenye matiti na makalio
kitu ambacho kimekuwa ni cha kiudhalilishaji sana” alilalamika Luiza
Mbutu.
Alitaja pia tabia ya wanamuziki wa kiume kwenye bendi kuponda mawazo ya
wanamuziki wa kike hasa pale wanapokuwa na wazo la kutunga nyimbo hali
ambayo imekuwa ikisababisha wao (wanaume) wawe wakipitisha nyimbo zao tu
na kuwaacha wanawake nyuma kwenye suala la utunzi wa nyimbo.
Aidha, alilalamikia baadhi ya wazazi ambao wamekuwa wakiwakataza watoto
wao wa kike kushiriki kwenye shughuli za sanaa hivyo kuwafanya wawe
wakitoroka usiku wa manane hivyo kushindwa kurudi majumbani baada ya
kuomba hifadhi kwa wanaume hivyo kuishia kupata mimba zisizo tarajiwa na
watoto wa mtaani.
Kuhusu hili la kuwadhalilisha wasanii wa kike, wachangiaji wengi kwenye
jukwaa walisema kwamba, rushwa za ngono zimekuwa zikisikika sana miongoni
mwa wasanii wa kike na mara nyingi kimekuwa ni kikwazo kwao kupata
mafanikio ya kisanaa.Walisema kwamba, kila wanapohojiwa wasanii wa kike
lazima walalamikie rushwa za ngono wanazoombwa na wasanii waliokwishapata
majina au wakuzaji sanaa (mapromota).
Akizungumzia maedeleo ya muziki wa dansi nchini,Rais wa Bendi ya FM
Academia ‘Wazee kwa Ngwasuma’ Nyoshi El Saadat alisema kwamba muziki huo
kwa sasa unakua hapa nchini ila tatizo ni wao wasanii kutokufaidika na
badala yake baadhi ya watu wamekuwa wakineemeka.
Kupitia kazi zao.
Alisema kwamba, zamani hakukuwa na maonyesho wala bendi nyingi hapa nchini
lakini kwa sasa hali ni tofauti kwani wasanii wanaonekana kuwa wengi kuku
mashabiki wakihamasika kila siku kuhudhuria maonyesho ya bendi.
Akiliahirisha Jukwaa la Sanaa,Katibu Mtendaji wa BASATA,Ghonche Marerego
alisema kwamba, lazima wasanii wa kike wawe wa kwanza kukataa
udhalilishaji na waoneshe wazi kukerwa na hali hiyo badala ya kufumbia
macho.
Alisema kwamba, kukomesha tabia ya unyanyasaji na udhalilishaji dhidi ya
wasanii wa kike huanza na wasanii wenyewe kwani haiingii akilini wakubali
kutuzwa kwa kuwekewa zawadi kwenye matiti au makalio yao.
“Wote sisi tuone kwamba ni jukumu letu na tupigane kuona maadili na
utamaduni wetu vikilindwa ili hata watoto watakaokuja huko mbele wakute
kitu cha kurithi” Alimalizia.

Comments