TEGETE, NURDIN 'WATIMULIWA' YANGA

JERRY TEGETE



NURDIN

KOCHA Mkuu wa klabu ya Yanga ya jijini Dar es Salaam, Mserbia Kostadin Papic jana aliwatimua katika mazoezi ya asubuhi ya timu hiyo, kiungo Nurdin Bakari na mshambuliaji Jerry Tegete yanayofanyika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.


Tukio hilo lililoshuhudiwa na baadhi ya mashabiki wa klabu hiyo, lilitokea baada ya wachezaji hao kuwasili uwanjani hapo wakiwa wamechelewa na kuwakuta wenzao wakifanya mazoezi, jambo ambalo lilimkera Papic, hivyo kuwazuia kujiunga na wenzao.

Wakati wachezaji hao wakiwa wanajiuliza cha kufanya, baadhi ya viongozi wa Yanga akiwamo Katibu wa Kamati ya Mashindano klabu hiyo, Emmanuel Mpangala waliwasihi wachezaji hao waende kumuomba msamaha kocha huyo.

Kutokana na hofu, wachezaji hao walisita kwa dakika kadhaa kabla ya Nurdin kumfuata uwanjani Papic na kuzungumza naye kwa muda, lakini msimamo wa kocha ulibaki kwamba ni marufuku wachezaji hao kujiunga na wenzao.

Papic aliyetua Jangwani katikati ya msimu uliopita akichukua nafasi ya Mserbia mwenzake Dusan Kondic, alihoji sababu zilizowafanya wakachlewa mazoezi tofauti na muda ambao wachezaji wote wanaufamu.

Kilichomkera zaidi Papic ni kutokana na wachezaji hao kurudia kosa hilo la kuchelewa ambalo walilifanya pia juzi na wakaonywa kuwa wasirudie tena, lakini jana asubuhihi wakarudia kosa hilo, hivyo kukawa hakuna msamaha tena.

Hadi mazoezi ya timu hiyo yakimalizika, wachezaji hao walikuwa hawajajiunga na wenzao hali ambayo imepongezwa na mashabiki waliokuwa uwanjani hapo kufuatilia mazoei ya timu yao kwa hoja kuwa, nidhamu kwa mchezaji ni kitu muhimu kwa mafanikio ya mchezaji na timu.

Comments