LLYOD NCHUNGA:MSOMI MWENYE KIU YA KULETA MAGEUZI YANGA


LYOD NCHUNGA

JULAI 18 ni siku muhimu na yenye thamani kubwa kwa wanachama wa klabu maarufu na kongwe ya Yanga ambayo wanachama wa klabu hiyo, hawapaswi kufanya makosa.


Ni siku ambayo wanachama wa klabu hiyo watakutana katika Ukumbi wa PTA uliopo kwenye viwanja vya Sabasaba, Mtoni kwa Azizi Ally, jijini Dar es Salaam.

Kukutana huko ni kufanya maamuzi kuhusu mwelekeo wa klabu hiyo kupitia uchaguzi mkuu utakaofanyika siku hiyo kuamua ni aina gani ya viongozi wapewe jahazi la kuongoza klabu hiyo kwa miaka minne.

Kama ni viongozi bora kwa maana ya weredi wa mambo na uadilifu uliotukuka mbele ya jamii ama bora viongozi wa kuirejesha Yanga kwenye migogoro.

Uchaguzi huu unafanyika baada ya kwisha kwa kipindi cha uongozi wa Imani Madega aliyeingia madarakani Mei 30, 2007.


Katika hili, naomba nisisitize kuwa uchaguzi ule (Mei 30, 2007), ni muhumu kuuumbuka kama alama ya kwisha kwa mgogoro uliokuwa umeiteza Yanga kwa szaidi ya miaka saba ukichukua sura ya Yanga- kampuni na Asili.

Upande wa kampuni ukiwa chini ya Francis Kifukwe na Yanga Asili chini ya Yusuf Mzimba, pande hizo zilisigana kwa muda mrefu hadi pale ulipozaliwa muafaka na hatimaye uchaguzi huo.

Ni muafaka ambao kwa kiasi kikubwa ulichangiwa na juhudi kubwa za mfadhili wa klabu hiyo, Yusuf Manji aliyeanza kuidhamini klabu hiyo Juni mwaka 2006.

Angalizo, wanachama wa Yanga wanapaswa kuelekea kwenye uchaguzi huku makovu ya mgogoro ule yakiwa funzo na chachu ya kutochagua viongozi wenye kuwagawa watu matabaka ili wawatawale (devide and Rule).

Katika hili, mgombea wa nafasi ya uenyekiti katika uchaguyzi huo, Lloyd Baharagu Nchunga ambaye kitaaluma ni mwanasheria, anasema akichaguliwa, atahakikisha wanachama wa klabu hiyo wanakuwa kitu kimoja.

Anasema kwa vile klabu hiyo ni mali ya wanachama, suala la umoja na mshikamano miongoni wao na viongozi wao kwa upande mwingine, ndiyo siri ya mafanikio.



“Katika hali ya kawaida, hata kama klabu itakuwa na safu nnzuri kiasi gani ya uongozi, kama wanachama hawatakuwa kitu kimoja, mafanikio hayawezi kupatikana,” anasema Nchunga.

Kwa upande wa kiuchumi, Nchunga anasema kama atachaguliwa, atatumia elimu yake na uhusiano wake mzuri na makampuni na taasisi mbalimbali kuanzisha SACCOS na baadaye Benki.

“Kama nitachaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Yanga nitaanzisha SACCOS ya Yanga na hatimaye Benki kwa lengo la kuwainua wanachama kiuchumi,” anasema.

Akizungumza katika mahojiano maalumu mwisho mwa wiki, Nchunga anayetumia kauli mbiu ya ‘Umoja Ushindi na mafanikio kwa maslahi ya Yanga,’ anasema amedhamiria kufanya mageuzi makubwa katika klabu hiyo.

Nchunga anasema ingawa furaha ya mwanachama, shabiki na mpenzi wa Yanga ni ushindi wa timu, lakini wanachama pia wanayo haki ya kupata manufaa zaidi ya ushindi, hivyo ni muhimu klabu yao ikatumika kuwakomboa kiuchumi.

Anasema mbali ya hilo, kama atachaguliwa atahakikisha anatumia ridhaa ya wanachama kufanya marekebisho ya katiba kwa kuboresha ama kuviondoa baadhi ya vipengele vilivyopitwa na wakati..

Akirejea kwa suala la umoja; Nchunga anakusudia kuwaungani wanachama na makundi yote ya Yanga ili kujenga Yanga moja na yenye nguvu.

Amesema, kama wanachama wa Yanga watampa ridhaa ya kuongoza, atawaunganisha wanachama kupitia matawi ya Yanga ili kuwe na mtiririko wa mawasiliano kutoka matawi hadi Kamati ya utendaji.

“Kwa mantiki hiyo, matawi yatapeana zamu ya kushughulikia masuala muhimu ya Yanga kwa mfano usimamizi wa mechi kwa utaratibu ambao utaonekana ni muafaka.

“Kwa mfano, Yanga inacheza mechi Songea, wanachama wa huko watakuwa na wajibu wa kuisimamia timu yao kwa kila kitu,” anasema.

Aidha, Nchunga anasema kitu kingine muhimu ni kuwepo kwa vikao vya mara kwa mara na kutoa taarifa kwa mujibu wa Katiba ili kuondoa uwezekano wa kuwepo kwa majungu ndani ya klabu.

“Pia kuweka wanayanga pamoja kwa kuondoa makundi ambayo naamini ndiyo yanaitokomeza klabu, pia nitayapa nguvu matawi ya Yanga yawajibike katika uongozi wa Yanga,” anaongeza.

USHINDI:
Nchunga anasema iwapo atafanikiwa kuwa mwenyekiti wa Yanga, akishirikiana na kamati ya utendaji, wataratibu timu za watoto na vijana na kuandaa vijana ambao wataichezea Yanga baadaye ili kupunguza gharama za usajili.

Pia, kusajili timu bora kwa michuano ya ndani na nje ya nchi, kumpa nafasi mkuu wa Kamati ya Ufundi kuhakikisha kuwa Kamati hiyo inafanya kazi zake kama inavyotakiwa.

“Tutaheshimu mbinu za kamati ya utendaji na kamati ya ufundi itaunda kamati maalum ya kuifuatilia timu inapocheza na kutoa tathmini ya mechi moja moja ili kujipanga kwa mechi ijayo,” anasema na kuongeza:

“Uongozi utasajili timu, kutafuta wachezaji chipukizi ambao wataichezea Yanga huku wengine wakipelekwa kwenye vituo maalum vya michezo utawasajili katika timu yetu ya wakubwa.

‘Kushirikisha wanachama kupitia matawi na vikosi kazi maalum ili kuhakikisha kila mechi tunashinda, kuunda kamati ya usalama na maadili ya kubaini mbinu chafu na kuzifanyia kazi mara moja.

‘Kutoa maslahi bora kwa wachezaji na kuwa karibu nao, nikiamini kuwa karibu na wachezaji, kutawapa faraja ya kujiona ni wenye thamani, hivyo kuitumikia Yanga kwa ari kubwa.

MAFANIKIO:
Kuendelea kushirikiana na mfadhili Yusuf Manji na wadhamini mbalimbali watakaojitokeza, hii ikimaanisha kuwa Yanga iwe katika mfumo wa kujitegemea na kumpunguzia mzigo Manji.

“Tunamshukuru Manji kwa kuifadhili klabu yetu kwa kiasi kikubwa hivyo tutaendelea kumuenzi kwa namaba moja ama nyingine sambamba na kutafuta wadhamini na wafadhili watakaosaidiana naye”.

‘Kuwa makini katika mikataba ya matangazo na logo ya yanga itumike kwa nafuaa ya klabu, kutumia eneo la klabu kiuchumi zaidi, pia kujenga uwanja wa mazopezi klabuni na kukusanya viingilio vyote’.

“Hiyo itahusisha kuukarabati uwanja wa Kaunda ili uweze kutumika katika mechi za ligi na hata za kimataifa, tayari kuna watu wameonyesha nia ya kufanya hivyo,” anaongeza

Aidha, kununua eneo la kijiji cha michezo cha Yanga, kuhakiki mali za Yanga na kuziweka katika mzunguko wa uzalishaji, pia kuongeza wanachama zaidi.

Nchunga anaongeza kuwa, chini ya uongozi wake, watatatufa klabu rafiki kutoka nje ya nchi katika bara la Afrika na Ulaya kwa ujumla ili kuinufaisha Yanga ambapo watashirikiana nazo kwa namna moja ama nyingine ikiwemo kubadilishana uzoefu na kupitia wachezaji.

Nchunga pia ameahidi kuwepo kwa kanuni bora za fedha na kutumia baadhi ya vianzio kwa miradi ya maendeleo, kutafanya mashindano na michezo mingi ya kirafiki ili kujenga ubora wa timu na kujiongezea kipato.

Anasema, uongozi utatafuta mawakala wa wachezaji na kuingia nao mikataba yenye maslahi kwa Yanga kwani hawataki mawakala kuwatumia isivyo wachezaji wa Yanga kwa manufaa yao.

“Lengo hapa ni kuondoa ubabaishaji wa mawakala uliojitokeza hivi karibu na matokeo yake wachezaji kuona uongozi unawabania, tumebaini nini cha kufanya ili kuondokana na hali hiyo,”anasisitiza

Mgombea huyo pia ameahidi kuwa kwa kushirikiana na viongozi wenzake na wanachama kwa ujumla, atafanya kila awezalo kuongeza idadi ya wanachama wa ndani hata nje ya nchi ili kuongeza wigo kama mtaji.

Je Nchunga ni nani?

Ni wakili wa kujitegemea akiendesha Kampuni yake ya Lloyd Advocates ya jijijini Dar es Salaam.

Akiwa na shahada ya Sheria aliyoipata Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kati ya mwaka 1989- 2003, alizaliwa mwaka 1967 na kupata elimu ya msingi katika shule ya Buhororo iliyopo Bukoba, Kagera mwaka 1974- 1980, kisha sekondari ya Ihungo mwaka 1981-1985, kisha kidato cha tano na sita Ilboru mwaka 1986 – 1988 na kisha JKT Makutupora mwaka 1988-1989.

Pia ni mwenye cheti cha utawala wa serikali za mitaa alichokipata katika chuo cha North Carolina kilichopo nchini Marekani.

Mwaka 1993 -2002, alikuwa mwanasheria katika Manispaa za Arusha, Halmashauri ya Wilaya ya Arumeri, Manispaa ya Dodoma, Tume ya jiji la Dar es Salaam na Manispaa ya Temeke.

Uzoefu wake katika soka:
Mwaka 1999- 2002 mjumbe wa Baraza la Michezo Wilaya ya Temeke, kabla ya mwaka 2004-2006 kuwa mjumbe wa kamati ya katiba ya kilichokuwa chama cha Soka (FAT) sasa (TFF) ambapo alishiriki kuiandika katiba iliyounda Shirikisho la Soka Tanzania TFF.

Nchunga pia alishiriki kutunga kanuni za uchaguzi mkuu wa TFF mwaka 2005 ambazo zilitumika kumchagua Rais wa sasa wa Shirikisho hilo, Leodger Chilla Tenga na wenzake.

Mwana 2005- 2008 alikuwa mjumbe wa kamati ya uchaguzi ya TFF.

Mwaka 2006 na kuendelea, amekuwa mjumbe wa kamati ya Uchaguzi ya Olimpiki Tanzania (TOC), mwaka 2007 alikuwa mjumbe wa kamati ya Ulinzi ya Baraza la vyama vya soka vya Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) katika michuano iliyoandaliwa na Baraza hilo.

2008- mpaka sasa amekuwa mjumbe wa kamati ya Nidhamu ya TFF, pia mwaka 2010 ameteuliwa kuwa mkufunzi wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) hapa nchini kuhusu utawala wa mpira wa miguu.

Comments