SIMBA NA YANGA ZINAONGOZA KWA KUUA VIPAJI VYA WACHEZAJI NCHINI

Na Dina Ismail
LICHA ya ukongwe  na umaarufu ilizonazo , vilabu vya Simba na Yanga vinaongoza kwa kuua vipaji vya wachezaji hapa nchini.
Ndiyo! Simba na Yanga ambazo ni mahasimu wa jadi nchini zinaongoza kwa kuua vipaji na kama wachezaji wasiposhtuka mapema tutapoteza vipaji vingi.
Timu hizo zenye umri wa miaka 80 tangu kuanzishwa kwake, zamani zilikuwa na historia nzuri ya kulea wachezaji wenye vipaji kwa muda mrefu tofauti na sasa.
Sijui ni utandawazi,  kukua kwa soka au  ulimbukeni  ndio kunakopelekea hali hiyo kwani hali hiyo imekuwa ikishika kasi kila uchwao.
Tanzania imejaaliwa kuna na wachezaji wenye vipaji vya hali ya juu lakini wengi wao wanajikuta wakipotea baada ya kujiunga Simba au Yanga.
Ukiangali kwa haraka haraka , kuna wale ambao walipitia katika vituo vya kukuza na kuendeleza soka za vijana au walipandishwa toka katika timu za vijana na kusajiliwa kuzicheza klabu hizo.
CHANZO:
Vilabu hivyo kuwa na uwezo mkubwa wa fedha, hufanya kila jitihada za kusajili wachezaji wazuri kwa lengo la kuimarisha vikosi vyao katika michuano mbalimbali.
Kamati za usajili za kila klabu zitaingia msituni kusaka wachezaji wazuri ambao wanaona watafaa kuzichezea.
Hapo  sasa kuna makundi mawili,  kuna walio kwa ajili ya kuzichezea tu klabu hiyo ili kujipatia umaaarufu na pesa na kuna kundi la ambao  wapo wenye malengo ya kufika mbali kupitia vilabu hivyo.
Katika hilo; mchezaji huyo atasota mchangani , wilayani na hata mkoa akijifua na hatimaye kuonwa na moja ya timu za Ligi Kuu na kusajiliwa.
Ataichezea  kwa nguvu zake zote timu yake hiyo iwe ya daraja la kwanza au ligi kuu.Lakini akili yake ni kusajiliwa Simba au Yanga!
Baada ya kusajiliwa na moja ya vigogo hao huko ataenda kukutana na changamoto nyingi ambazo bila umakini atajikuta ndio basi tena.
Kuna ambaye atafanikiwa kuingia kikosi cha kwanza, kuna atakayebaki  kwa ajili ya mazoezi tu, sasa bila kuchekecha akili ndio itakuwa mwisho wake.
Kundi la Pili linaundwa na wachezaji ambao wanajielewa.Haijulikani kapitia njia ipi mpaka kusajiliwa Simba au Yanga.
Yeye akili yake ni kufika mbali katika medani ya soka, huyu hata akikumbana na changamoto kwenye vilabu hivyo atakabiliano navyo na mwish wa siku atafanikiwa tu.
Hii ndio aina ya wachezaji wanaofika mbali kwani baada ya kuingia katika utawala wa Simba na Yanga.
Na tumeshudia kuwepo kwa baadhi ya wachezaji ambao  hucheza kwa nguvu zote hasa pale timu yake inakapokutana na Simba au Yanga,atafanya kila awezalo ili aweze kuvutia na kesho atafutwe.
Hapo inaonesha lengo la wachezaji wengi ni kuzichezea Simba au Yanga na sio kuwa mchezaji mwenye lengo la kufika mbali.
Tabu inakuja atakaposajiliwa changamoto atakazokutana nazo Simba au Yanga ndizo zitakazomfanya abaki kikosi cha kwanza au asugugue benchi na kujibidiisha zaidi ili siku moja afanikiwe kusonga mbele.
Sio rahisi  kupata namba katika kikosi cha kwanza kama alivyofikiria kabla.Hiyo inatokana na kila idara kusheheni wachezaji wazuri na wenye uwezo wa hali ya juu.
Hapo inakuwa kama wanacheza bahati nasibu kwani kila mwenye bahati ndiye atakayekuwa chagua la kocha na hivyo kupata  namba katika kikosi cha kwanza.
Kwa mchezaji mwenye malengo kama hatobahatika kuingia kikosi cha kwanza, atashtuka mapema na kujiongeza zaidi ili aweze kutimiza lengo lililompeleka hapo.
Lakini kuna watakaobweteka kwa kuendelea kusugua benchi, mradi mwisho wa mwezi ATM inasoma yeye hajali.Mwisho wa siku unakumbwa na fagio mwisho wa msimu.
Wachezaji wengi wa Tanzania wanapotea baada ya kuingia Simba au Yanga  kwani huko watakutana na kila aina ya tabia ambazo zinasababishwa na umaarufu walionao, uwezo na uzoefu.Hivyo baadhi hujisahau!
Suluhisho

Mchezaji anatakiwa kutumia akili ya  ziada ili kuweza kufika mbali kinyume na hapo itabaki katika historia tu.

Comments