WAKALI HAWA WA SOKA WAMEPOTEA NA UMAHIRI WAO


Joseph Kaniki 'Golota'


Na Dina Ismail

TANZANIA imejaliwa kuwa na vipaji vya hali ya juu katika michezo na hasa mpira wa miguu lakini imeshindwa kufanya vema katika medani za kimataifa.
Wengi wa wachezaji ambao walibahatika kufikia hatua ya kucheza hadi  timu ya Taifa  wameshindwa kudumu kwa muda mrefu kama ilivyo kwa nchi nyingine zilizoendelea licha ya kuwa na uwezo mkubwa.
Haijajulikana sababu hasa ya wachezaji  wengi wazuri kutodumu kwa muda mrefu kucheza soka  ushindani licha ya umri wao kuwa bado unaruhusu na pia kuwa na vipaji.
Ukiangalia kwa haraka haraka kinachopelekea hali hiyo ni utovu wa nidhamu pamoja na  mfumo mzima wa uongozi wa soka hapa nchini.
Hali hiyo imekuwa ikishika kasi katikati  ya  miaka ya 2000 ambapo tumeshuhudia wachezaji wengi wazuri ambao walikuwa wakifanya vema katika timu mbalimbali na hasa za Ligi Kuu.
Katika makala hii tutawazungumzia  baadhi ya wachezaji  waliopo kwenye kundi hilo ambao kutokana na changamoto mbalimbali  huenda  mpaka hii leo wangekuwa ni baadhi ya nyota waliomo kwenye kikosi cha timu ya Taifa au kucheza soka la kulipwa.

Emmanuel Gabriel Mwakyusa:
Jina lake lilipata umaarufu zaidi mwanzoni mwa miaka ya 2000 aliposajiliwa na Klabu ya Simba kutoka klabu ya Nazareth ya Njombe.
Mshambuliaji huyo mwenye nguvu na kasi ya ajabu awapo uwanjani alikuwa ni mmoja ya wachezaji wa Simba ambao waliiwezesha kufanya vema kwenye michuano ya kitaifa na Kimataifa.
Gabriel ambaye alipachikwa jina la Batigol akifananishwa  na nyota wa Kiargentina Gabriel Batistuta ‘Batigol’, aliitumikia klabu ya Simba kabla ya kuuzwa katika klabu ya Fanja ya Oman.
Nyota huyo pia amepata kuzitumikia klabu za AFC ya Arusha na Prisons ya Mbeya kwa nyakati tofauti, tangu alipoondoka Simba nyota yake ilififia licha ya umahiri aliokuwa nao.
Batigol ambaye alijizolea umaarufu zaidi kutokana na kufunga mabao kwa kichwa kupitea kwake pia kulichangiwa pia baada ya kupata majeraha kwa muda mrefu na hivyo baada ya kupona ameshindwa kurudi katika fomu.

Amir Maftah:
Ni mmoja ya mabeki mahiri hapa nchini ambaye alipata kuzichezea klabu kongwe hapa nchini, Simba na Yanga kwa nyakati tofauti.
 Maftah aliyesajiliwa Simba mwaka 2011 baada ya kutemwa Yanga ni mmoja ya mabeki mahiri nchini ambaye amekuwa akitumika vema katika klabu anazozitumikia pindi awapo uwanjani.
Beki huyo wa kushoto ambaye pia alipata kuitumikia timu ya Taifa kwa nyakati tofauti, aliibukia katika klabu ya Pamba ya Mwanza kwa sasa anaitumikia klabu ya Friends Rangers ambayo inashiriki Ligi daraja la kwanza.
Licha ya umahiri na kipaji alichonacho,  Maftah ni mmoja ya wachezaji wazuri ambao bado hajafikia hatua ya kuangukia katika  ligi daraja la kwanza.

Joseph Kaniki ‘Golota’:
Mashabiki wa soka bado wanalikumbuka sana jina lake kutokana na umahiri alikuwa nao enzi akiicheza soka hapa nchini katika klabu ya Simba na timu ya Taifa.
Umahiri wa mshambuliaji huyo mwenye nguvu na kasi awapo uwanjani ulimuwezesha kuipa ushindi mnono timu yake pindi anapopangwa.
Akiwa ni mmoja ya wachezaji waliochangia mafanikio ya Simba katika miaka ya mwanzoni mwa 2000, soka lake lilianza kushuka baada ya kuhusishwa na vitendo vya utovu wa nidhamu.
Baada ya kutoka Simba, alizichezea kwa nyakati tofauti klabu za Mtibwa Sugar ya Morogoro, Al tali’aa ya Misri na Rayon ya Rwanda na klabu ya daraja la pili KonyaSpor (KIF) nchini Sweden.
Golota ambaye kwa sasa anatumikia kifungo cha miaka saba na nunsu nchini Ethiopia baada ya kukamatwa mwaka 2012 nchini humo akiwa na dawa za kulevya ni mmoja ya wachezaji ambao wangeweza kuwa kwenye  timu kubwa za ligi kuu akicheza soka la ushindani mpaka sasa.

Nsa Job Mahinya:
Ni mmoja ya wachezaji wenye vipaji vya aina yake ambaye umahiri wak ulimuwezesha kujipatia umaarufu mkubwa nchini.
 Job ambaye alipata kuzitumikia klabu kongwe za Simba na Yanga kwa nyakati tofauti ni mmoja ya washabuliaji wanaotumia vema uwezo wao wapatapo nafasi uwanjani.
Umahiri wake ulimuwezesha kuitumikia pia timu ya Taifa kwa nyakati tofauti lakini jina lake lilipotea baada ya kupata majeruhi akiwa klabu ya Azam Fc.
Pia amepata kuzitumia klabu za Azam Fc, Moro United na African Sports ya Tanga.

Boniface Pawasa:
Mashabiki wa soka nchini bado wanamkumbuka beki huyu kisiki wa zamani wa klabu ya Simba na timu ya Taifa.
Pawasa ambaye alijunga na Simba mwanzoni mwa miaka ya 2000 akitokea CDA ya Dodoma ni mmoja ya wachezaji waliokuwa tishio uwanjani kutokana na kuwa na uwezo mkubwa wa kuhimili vishindo vya timu pinzani .
Hata hivyo nyota ya mchezaji huyo ilianza kupotea katikati ya miaka ya 2000 baada ya Simba kumsimamisha kabla ya kumuacha kabisa kwa madai ya utovu wa nidhamu  na kisha nyota huyo kutimkia nchini Rwanda na Uarabuni kucheza soka la kulipwa kwa nyakati tofauti.
Pawasa alipata kuwa mmoja ya wachezaji wa kwanza ambao waliipandisha Azam Fc kutoka Ligi Daraja la kwanza hadi Ligi Kuu Bara.
Kwa kipaji alichonacho angekuwa ni mmoja ya wachezaji ambao wangekuwa gumzo katika medani ya soka mpaka sasa.
PAwasa kwa sasa hachezi soka ya ushindani huku akijikita zaidi katika kujiendeleza katika hatua ya ukocha wa soka.

Victor Costa:
Jina lake halisi ni Victor Nampoka, ni moja ya mabeki wenye nguvu na uwezo mmkubwa uwanjani.
Costa  jina lake lilipata umaarufu zaidi mwanzoni mwa mwaka 2000 akiwa na klabu ya Simba ambapo mwaka 2003 alikuwa ni mmoja ya wachezaji wa timu hiyo waliofanikiwa kuivua ubingwa Afrika Zamalek ya Misri.
Nyota huyo ambaye pia alikuwa ni mmoja ya wachezaji waliokuwa wakiichezea timu ya Taifa ya Tanzania alianza kupotea kwenye mwaka 2005 baada ya kuumia kisigino akiitumikia timu ya Taifa.
Baada ya kujiuguza kwa muda mrefu na kupona alitimkia nchini Msumbiji na kwenda kuitumikia klabu ya  Agasabe Disongo kwa misimu kadhaa, kabla ya kurejea tena nchini na kujiunga na Simba.
Hata hivyo, jina la Costa limekuwa likipotea taratibu tangu alipoumia.
Costa aambaye kwa sasa yupo Visiwani Zanzibar akiwa na timu yake ya zamani ya Jang’ombe kama kocha mchezaji, alipata kuzicheza pia timu za Mtibwa Sugar, Mwadui Fc na Ashanti United.
Ramadhan Chombo ‘Redondo’:
Kwa sasa anakipiga katika klabu ya Mbeya City inayoshiriki Ligi Kuu Bara.
Redondo ni mmoja ya viungo mahiri ambao walipata kuwika miaka ya nyuma na umahiri wake ulimfanya kuchaguliwa kuichezea timu ya Taifa ya Tanzania.
Nyota yake ilianza kung’ara mwaka 2000 akiwa katika kituo cha kukuza vipaji cha DSM youth Centre kablya ya kutimkia nchini Norway mwaka 2003 alipojiunga na klabu ya daraja la pili  ya Lyngdal na kisha kerejea nchini mwaka 2007 alipojiunga na Ashanti United.
Kutokana na umahiri wake,Redondo ambaye pia humudu nafasi ya winga alinyakuliwa na Simba mwaka 2008 ambako alidumu nayo hadi 2010 na kisha kerejea tena Azam Fc na baadaye kutimkia nchini Msumbiji na kisha kurejea nchini alipojiunga na Mbeya City.

Kipaji na uwezo mkubwa alionao Redondo ni mmoja ya wachezaji ambao wangekuwa juu kwa sasa kama si kuwepo kwa changamoto kwenye medani ya soka.

Comments