RAGE AMKINGIA KIFUA KIBADENI

RAGE

CHANZO:Liwazozito blog
MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amesema atawachukulia hatua za kinidhamu, viongozi watakaobainika kuingililia kazi na majukumu ya benchi la ufundi la timu hiyo.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Tabora jana, Rage alisema hakuna kiongozi anayeruhusiwa kumpangia timu Kocha Mkuu wa timu hiyo, Abdalla Kibadeni.
Rage ametoa tishio hilo baada ya Kibadeni kukaririwa wiki hii akisema kuwa, baadhi ya viongozi wa klabu hiyo wamekuwa wakimshinikiza kuwachezesha wachezaji wanaowapenda.
Kwa mujibu wa Kibadeni, viongozi hao walitaka kuingilia majukumu yake kabla ya mchezo wao wa ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Simba, uliochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
"Kibaden ni kocha halali wa Simba,ana mkataba na amesomea fani hiyo, hivyo kama kuna kiongozi ameingilia kati majukumu yake, tutamshughulikia,"alionya Rage.
Wachezaji, ambao Kibadeni amelalamika kwamba, amekuwa akishinikizwa kuwachezesha ni pamoja na kiungo, Abdulharim Humud, ambaye alionyesha kiwango cha chini katika mechi dhidi ya Yanga.
Katika mechi hiyo, Simba na Yanga zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya mabao 3-3. Yanga ilikuwa mbele kwa mabao 3-0 baada ya dakika 45 za kwanza, lakini Simba ilizinduka kipindi cha pili na kusawazisha.

Comments