TUSKER FC YAJA KUZIVAA SIMBA, YANGA WIKIENDI HII


TIMU ya soka ya Tusker inayoshiriki Ligi Kuu nchini Kenya inatarajiwa kuwasili nchini kesho  kwa ajili ya kuwakabili miamba ya soka nchini Simba na Yanga, imefahamika.
Tusker inatarajiwa kucheza na mabingwa wa Ligi Kuu Bara, Yanga jumamosi kabla ya Jumapili kuwakabili Simba ambapo michezo yote itafanyika katika uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Ofisa Habari wa Chama cha Soka mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) iliyoandaa michezo hiyo Mohammed Mharizo alisema maandalizi ya michezo hiyo yanakwenda vema.
Alisema lengo la kuandaa michezo hiyo ni kuzipa maandalizi timu hizo hususani katika kipindi hiki ambapo ligi imesimama kwa ajili ya kuipisha timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ ambayo ipo katika maandalizi ya mechi yake ya Mchujo wa kombe la Dunia dhidi ya Gambia utakaopigwa ugenini Septemba 7.
Mharizo aliongeza kuwa tusker inatarajiwa kuja na nyota wake wote kwa ajili ya michezo hiyo ambapo kama ilivyo kwa Simba na Yanga, itawasaidia na wao kujinoa kwa ajili ya ligi ya kwao.
Wakati Simba itautumia mchezo huo kujiandaa na mechi yake dhidi ya Mtibwa Sugar utakaopigwa Septemba 14 katika dimba la Taifa jijini Dar es Salaam, Yanga itakuwa inajinoa kwa mechi yake dhidi ya Mbeya City utakaofanyika Septemba 14 katika Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.

Kwa upande wa Tusker, itakuwa na kibarua kigumu cha ligi ya kwao ambapo inatarajiwa kucheza na Gor Mahia,Septemba 15. 

Comments