SIMBA YAUA 2-0, YANGA NA AZAM ZABANWA MIKOANI

Na Mahmoud Zubeiry, Mbeya, IMEWEKWA SEPTEMBA 14, 2013 SAA 12:45 JIONI
LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara imeendelea leo kwenye viwanja tofauti, huku mabingwa watetezi, Yanga SC wakilazimishwa sare ya 1-1 na wenyeji Mbeya City na Simba SC wakishinda 2-0 dhidi ya Mtibwa Sugar, wakati Azam FC imetoa sare ya 1-1 na wenyeji Kagera Sugar.  
Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, mabingwa watetezi walilazimika kusubiri hadi dakika ya 82 kujihakikishia japo kupata pointi moja mbele ya Mbeya City.
Mbeya inayofundishwa na Juma Mwambusi, ndiyo walioanza mchezo huo kwa kasi wakishambulia zaidi kutokea pembeni na kulitia misukosuko lango la Yanga SC.

Mshambuliaji wa Yanga SC, Didier Kavumbangu akiruka kupiga kichwa mbele ya mabeki wa Mbeya City leo Uwanja wa Sokoine.

Mbeya inayofundishwa na Juma Mwambusi, ndiyo walioanza mchezo huo kwa kasi wakishambulia zaidi kutokea pembeni na kulitia misukosuko lango la Yanga SC.
Pamoja na kocha Mholanzi, Ernie Brandts kuanzisha washambuliaji watatu, Didier Kavumbangu, Hussein Javu na Said Bahanuzi, lakini kuzidiwa kwa timu yao katika safu ya kiungo kuliwafanya wasiwe na madhara.
Hata hivyo, hadi mapumziko hakuna timu iliyofanikiwa kuona lango la mwenzake na kipindi cha pili, Mbeya waliingia kwa kasi zaidi na kufanikiwa kupata bao dakika ya nne tu tangu kuanza kipindi hicho.
Krosi maridadi ya Hassan Mwasapili kutoka wingi ya kushoto iliunganishwa vizuri kwa kichwa na Mwagane Yeya ‘Morgan’ na kumpita kipa Ally Mustafa ‘Barthez’ kama amesimama.
Baada ya bao hilo, Yanga walicharuka na kuanza kucheza kwa nguvu na kushambulia zaidi na almanusra mchezo uingie dosari dakika ya 58, baada ya Didier Kavumbangu kuuwahi mpira aliokuwa akiuchezea kipa wa Mbeya City, David Burhan na kuutumbukzia nyavuni, lakini refa akakataa bao.
Kipa huyo alidaka shuti la Nizar Khalfan na kuanza kuuchezea mpira kwa madaha akiudundaduna huku ameinama, ndipo Kavumbangu akamsogelea na kwa mchecheto mpira ukamtoka kipa huyo mikononi na mshambuliaji huyo wa Yanga akawahi kuusukumia nyavuni.          
Baada ya refa Andrew Shamba kukataa bao hilo, wachezaji wa Yanga walimtia kashikashi kidogo, kabla ya kuendelea na mchezo. 
Timu ziliendelea kushambuliana kwa zamu, lakini mabadiliko yaliyofanywa na kocha Brandts kuwaingiza mfululizo Jerry Tegete na Oscar Joshua kuchukua nafasi za Nizar na Bahanuzi kuliongeza uhai Yanga na matunda yake ni kusawazisha bao dakika ya 82 kupitia kwa Kavumbangu, akimalizia krosi David Luhende.
Kwa matokeo hayo, Yanga inafikisha pointi tano baada ya kucheza mechi tatu, ikitoa sare mbili na kushinda moja, sawa na Mbeya City ambao pia wana pointi tano sasa baada ya sare mbili na kushinda mechi moja, zote nyumbani.
Mapema mashabiki wa Mbeya City walilitupia mawe basi la Yanga wakati linaingia uwanjani na kusababisha kioo cha mbele upande wa dereva kuvunjika na pia kumjeruhi dereva huyo.
Mwenyekiti wa Yanga SC, Yussuf Manji alikuwa jukwaani kushuhudia mchezo huo pamoja Makamu Mwenyekiti wake, Clement Sanga na Wajumbe wa Kamati ya Utendaji, Isaac Chanji na Mussa Katabro.
Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite, David Luhende, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Athumani Iddi ‘Chuji’, Nizar Khalfan/Jerry Tegete dk59, Frank Domayo, Didier Kavumbangu, Hussein Javu na Said Bahanuzi/Oscar Joshua dk59.
Mbeya City; David Burhan, John Kabanda, Hassan Mwasapili, Deogratius Julius, Antony Matogolo, Yohana Morris, Mwagane Yeya, Steven Mazanda, Paul Nonga/Fidelis Castor dk82, Deus Kaseke, Yussuf Willson/Alex Sethi dk 59.   
Katika mechi nyingine za Ligi hiyo, Simba SC iliiendeleza wimbi la ushindi baada ya kuilaza Mtibwa Sugar 2-0.
Hadi mapumziko, hakuna timu iliyofanikiwa kupata bao na kipindi cha pili, ndipo Wekundu wa Msimbazi walipong’ara, Henry Joseph akianza kufunga dakika ya 70 na Betram Mombeki akafuatia dakika ya 90.
Simba SC; Abbel Dhaira, Nassor Masoud ‘Chollo’, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Kaze Gilbert, Joseph Owino, Jonas Mkude, Twaha Ibrahim/Betram Mombeki dk64, Said Ndemla/Henry Joseph dk55, Amisi Tambwe, Amri Kiemba na Haroun Chanongo/Ramadhan Singano dk77. 
Mtibwa Sugar; Hussein Sharrif ‘Casillas’, Hassan Ramadhani, Paul George, Dickson Daudi, Salim Abdallah, Shaaban Nditi, Ally Shomary, Masoud Mohamed/Awadh Juma dk58, Juma Luizio/Mussa Mgosi dk46, Shaaban Kisiga/Abdallah Juma dk75na Vincent Barnabas.
Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, Themi Felix Buhaja alitangulia kuifungia Kagera Sugar dakika ya 25 kabla ya Khamis Mcha ‘Vialli’ kuisawazishia Azam FC dakika ya 55. 
Katika mechi nyingine Coastal Union ilitoka sare ya bila kufungana na Tanzania Prisons Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, Ruvu Shooting iliifunga 1-0 Mgambo Shooting bao pekee la Elias Maguri dakika ya 53 Uwanja wa Mabatini mkoani Pwani, Oljoro JKT ilitoka sare ya 1-1 Rhino Rangers Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha, wenyeji wakilazimika kusawazisha dakika ya 27 kupitia kwa Amiri Hamad baada ya Saad Kipanga kutangulia kuwafungia wageni dakika ya tano, wakati Ashanti United ililala 1-0 mbele ya JKT Ruvu, Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam bao pekee la Amos Mgisa dakika ya 81.
Matokeo hayo, yanamaanisha JKT Ruvu inaendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi zake tisa baada ya kushinda mechi zote tatu, ikifuatiwa na Simba SC katika nafasi ya pili yenye pointi saba. Timu nyingi zimefungana kwa pointi tano katika nafasi ya tatu, zikiwemo Yanga, Azam na Coastal Union.

Comments