SIMBA KUKIPIGA NA MABINGWA WA ZANZIBAR KESHO

KESHO Ijumaa, Septemba 6 mwaka 2013, klabu ya Simba itacheza mechi ya kirafiki na mabingwa wa soka wa Ligi Kuu ya Zanzibar, KMKM, katika mechi itakayochezwa katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Lengo kuu la mechi hiyo ni mazoezi kwa Simba ya kujiandaa na mchezo wake dhidi ya Mtibwa Sugar uliopangwa kufanyika Septemba 14 mwaka huu.
Kikosi kamili cha KMKM kimewasili jijini Dar es Salaam tayari na leo saa tano na nusu kamili nahodha wake, Abdi Kassim Babi na kocha mkuu wa timu hiyo wanatarajiwa kuzungumza na waandishi wa habari katika mgahawa wa City Lounge katikati ya jiji.
Simba inaendelea na mazoezi yake jijini na wachezaji wake wote wapo katika hali nzuri na tayari kwa ajili ya mechi hiyo.

Mechi hiyo itaanza majira ya saa 11 jioni ili kuwezesha watu wengi kwenda uwanjani kutazama mechi hiyo ikizingatiwa kuwa Ijumaa ni siku ya kazi.

Ezekiel Kamwaga
Ofisa Habari
Simba SC


EEE

Comments