WALLACE KARIA AWEKEWA PINGAMIZI UCHAGUZI TFF

Wanamichezo wawili walioomba kuwania uongozi kwenye uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) utakaofanyika Oktoba 27 mwaka huu wamewekewa pingamizi.
Waliopingwa ni Wallace John Karia anayeomba kupitishwa kuwania urais na Vedastus Kalwizira Lufano anayewania ujumbe wa Kamati ya Utendaji kupitia Kanda Namba Mbili ambayo ni mikoa ya Mara na Mwanza. Anyempinga Karia ni Shamsi Rashid Kazumari wa Dar es Salaam wakati Lufano anapingwa wa Samwel Nyalla wa Mwanza.
Pamoja na mambo mengine, Kazumari anampinga Karia kwa madai kuwa akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Ligi, aliwashawishi wajumbe wenzake kuingia mkataba na Azam Tv wakati akijua kamati hiyo ni ya muda, hivyo haina nguvu za kisheria kusaini mkataba huo.
Naye Nyalla ambaye pia ni mmoja wa wanamichezo waliojitokeza kuwania ujumbe kupitia Kanda hiyo anampinga Lufano kwa madai hana uzoefu wa miaka mitano katika uongozi wa mpira wa miguu.

Kamati ya Uchaguzi ya TFF chini ya Mwenyekiti wake Hamidu Mbezeleni itakutana kesho (Agosti 28 mwaka huu) saa 4 kamili asubuhi kusikiliza pingamizi hizo ambapo wawekaji pingamizi na waliopingwa wanatakiwa kufika wenyewe ndani ya muda kwa vile uwakilishi hautakiwi.

Comments