TIKETI ZA ELEKTRONIKI KUANZA KUTUMIKA SEPTEMBA 18

Tiketi za elektroniki zitaanza kutumika katika mzunguko wa nne wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) utakaoanza Septemba 18 mwaka huu. Tayari benki ya CRDB ambayo ndiyo ilishinda tenda hiyo imeshakamilisha ufungaji wa vifaa kwa ajili ya matumizi ya tiketi hizo katika viwanja vyote. 
Hivi sasa Serikali ambayo ndiyo inamiliki Uwanja wa Taifa, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) pamoja na CRDB zinashughulikia mfumo wa tiketi hizo kwenye uwanja huo ambao ndiyo ulikuwa haujakamilika kwa matumizi katika upande huo. 
Mfumo (system) iliyoko kwenye uwanja huo inapishana na ule utakaotumiwa na CRDB, hivyo pande husika zinashughulikia suala hilo ili mifumo hiyo iweze kuingilia. 
Pia mashine za kuchapia (printer) kwa ajili ya tiketi ambazo CRDB wameziagiza kutoka nje ya nchi zinatarajiwa kuwasili mwishoni mwa mwezi huu. 
Hivi sasa CRDB inashughulikia ufungaji wa vifaa vya matumizi ya tiketi za elektroniki iwemo turnstiles kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi ambao mwanzoni hakuwemo kwenye mpango huo kutokana na Mkoa wa Tabora kutokuwa na timu ya Ligi Kuu.

Comments