MWINYI KAZIMOTO ASAINI MWAKA MMOJA NA NUSU AL MARKHIYA, WAIPANDISHIA DAU SIMBA

ALIYEKUWA kiungo wa Simba Mwinyi Kazimoto jana amesaini mkataba wa mwaka mmoja na nusu kwa ajili kuitumikia klabu ya Al Markhiya SC ya Doha, Qatar.
Habari za uhakika kutoka Qatar zinaeleza kwamba, Kazimoto amesaini mkataba baada ya kufaulu majaribio yake, sambamba na kukubaliana na uongozi ofa aliyopewa.
Imeelezwa kwamba, hatua ya Kazimoto kusaini mkataba huo imekuja baada ya uongozi wa timu hiyo kuongeza dau la kumnunua baada ya awali kugomea kwa madai kuwa halilingani na thamani waliyomnunulia.
Chanzo hicho kimeeleza kwamba, Al Markhiya iliwaangukia Simba kwa dau waliloafikiana kutokana na ukweli kwamba kwa sasa ipo katika hali mbaya ya kifedha na hasa ikizingatiwa kuwa wanahitaji kusajili wachezaji watakaoipandisdha tena daraja.
“Unajua timu imeshuka daraja hivi karibuni sasa wanajiimarisha kwa kusajili wachezaji wazuri na fedha waliyonayo haitoshelezi hivyo wameiomba Simba ipokee hicho walichonacho,”kilieleza chanzo hicho.
Juzi uongozi wa Simba kupitia kwa msemaji wake Ezekiel Kamwaga ulisema umeitupilia mbali ofa iliyotumwa na klabu hiyo kwa madai kuwa ni ya kipuuzi, huku ikidai pia Kazimoto ana maswali kwanza ya kujibu kwa Watanzania na mashabiki wa Simba kwa ujumla.
Simba pia ilidai inakusudia kuketi na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa ajili ya kumjadili nyota huyo kwa kitendo chake cha kutoroka nchini.

Kazimoto ambaye alisajiliwa na Simba mwaka juzi kutokea JKT Ruvu, alitoroka nchini akiwa na timu timu ya Taifa iliyokuwa ikijiandaa na mechi yake ya kufuzu fainali za Afrika zinazoshirikisha nyota wanaocheza ligi za ndani (CHAN) dhidi ya Uganda ‘The Cranes’

Comments