Na Dina Ismail
HIVI karibuni mlinda mlango namba moja Tanzania, Juma Kaseja amepata
kuwa gumzo katika vyombo mbalimbali vya habari hapa nchini.
Gumzo hilo linatokana na uongozi wa timu ya soka ya Simba kutangaza
kutomuongeza mkataba wa kuendelea kuichezea klabu hiyo baada ya kuitumikia kwa
karibu miaka tisa.
Uongozi wa Simba uliamua kuvunja ukimya kwa kutangaza kutomsaini tena
Kaseja baada ya kuwepo sintofahamu iliyokuwa ikiendelea ndani ya klabu hiyo
baada ya mkataba wake kumalizika mwezi Mei.
Kwamba, viongozi wa Simba waligawanyika makundi mawili kuhusiana na
suala la Kaseja, ambaye alikuwa pia nahodha wa timu hiyo ambapo kuna waliotaka
aongezwe mkataba na kuna waliotaka asiongezwe.
Ilifikia hatua hata vikao vyao kuvunjika baada ya suala la Kaseja
kuibuka, kwani viongozi walijikuta katika mabishano na mwisho wa siku kushindwa
kupatikana mwafaka.
Hata hivyo hakukuwa na sababu ya msingi ya viongozi hao kugawanyika na
hasa katika suala la kutomtaka tena katika klabu yao zaidi ya kutoa sababu
zisizo na mashiko yoyote.
Kingine ni kwamba, hata kocha mkuu wa timu hiyo Abdallah ‘King’
Kibaden naye alipigilia msumari juu ya
mustakabali wa Kaseja na kusema kuwa asingekuwa tayari kuifundisha Simba iwapo
Kaseja angeongezwa mkataba.
Kibaden naye alikataa uwepo wa Kaseja ndani ya kikosi chake bila ya
kutoa sababu, kama ni kuwa ameshuka kiwango, mtovu wa nidhamu au lingine lolote.
Sakata hilo lilikuwa likichukua sura mpya kila kukicha, wapo waliodai
Kaseja kutaka dau kubwa ili kusaini mkataba mpya, wapo waliodai nyota huyo
anataka mkataba wa miaka miwili wakati uongozi unataka kumpa mwaka mmoja,
lakini katika hilo uongozi ulidai kuwa haujaketi chini kuzungumza na Kaseja juu
ya hayo.
Kuachwa kwa Kaseja haikuwa jambo la kushitukiza hata kidogo bali ni
mkakati uliopangwa kwa muda mrefu na hatimaye kuhitimishwa katikati ya wiki
hii.
Kila mpenda soka hapa nchini anafahamu kiwango alicho nacho Kaseja na
yaliyokuwa yakitokea hapa katikati, inawezekana ni kughafirika kulikotokana na
kuchanganywa na hali tete iliyokuwa ikimuandama ndani ya klabu yake.
Kaseja ni mmoja ya wachezaji wachache sana wanaoithamini kazi yao na
ubora wake ulianza kuonekana tangu alipokuwa sekondari ya Makongo, timu za
Vijana kabla ya kusajiliwa na timu za Ligi Kuu ameweza kulinda kiwango chake
kwa kiasi kikubwa.
Tofauti na wachezaji wengine, Kaseja amekuwa ‘Tanzania One’ kwa muda
mrefu na alikomaa zaidi katika namba hiyo baada ya kustaafu kwa aliyekuwa
‘Tanzania One’ Mohammed Mwameja na kurithi nafasi yake ndani ya Simba tangu
mwaka 2003.
Kaseja pia amekuwa chaguo namba moja katika kikosi cha timu ya Taifa
tangu akizichezea timu za vijana hadi ile ya wakubwa na ni mara chache sane
makocha walishindwa kumpanga katika kikosi cha kwanza.
Lakini Kaseja alianza
kuonekana si lolote baada ya timu yake ya Simba kuanza kufanya vibaya katika
ligi kuu bara na michuano ya kimataifa misimu miwili iliyopita na ndipo jina
lake lilianza ‘kunuka’.
Kwa wenye kumbuku nzuri, Kaseja pamoja na baadhi ya wachezaji waliokuwa
katika kikosi hicho kwa muda mrefu kama Mussa Hassan Mgosi, Mohammed Banka,
Victor Costa, Haruna Moshi ‘Boban’, na
wengineo walisukiwa mpango wa kuondolewa kundini.
Haikuwa kwa hao tu bali mkakati huo uliwahusu hata baadhi ya wachezaji
wengine ambao walihamia katika timu hiyo kama Amir Maftah, Juma Nyoso, Mwinyi
Kazimoto na wengineo huku ikidaiwa
kutaka kuondoa wakongwe kwani kwa wakati huo Simba iliweka mkakati wa kuwatumia
vijana zaidi.
Kwamba wachezaji hao wamekuwa ‘virusi vibaya’ ndani ya timu hivyo
kuendelea kuwa nao italeta athari kwa wachezaji chipukizi ambao walianza
kuonesha ustawi mzuri ndani ya Simba.
Na ndipo walianza kuondolewa mmoja baada ya mwingine baada ya
kusimamishwa kwa muda usiojulikana kwa madai ni watovu wa nidhamu (kwa sababu
mbalimbali) na kupotezewa mpaka mkataba kuisha.
Wengine walipelekwa kucheza kwa mkopo katika vilabu mbalimbali mradi tu
waondoe virusi, lakini kwa Kaseja ilishindikana kwani hawakupata sababu ya
kumtoa kafara kabla ya zamu yake kufika wiki iliyopita baada ya ‘kuvuliwa
gwanda’ lake.
Baada ya uongozi kutangaza rasmi kuachana naye, ndipo ikabainika
kwamba, chanzo ni mechi ya funga dimba ya ligi kuu bara dhidi ya mahasimu wao
Yanga ambapo Simba ilitandikwa mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa Mei 18 kwenye
Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Taarifa za ndani kutoka Simba zinadai kuwa, Kaseja aliihujumu Simba na
matokeo yake timu ilipoteza mchezo huo ambapo yeye alikaa langoni.
Kwa mantiki hiyo, kitendo kile
kiliwaudhi sana viongozi kwani mabao aliyofungwa yalionekana dhahiri kuwa
yalitokana na uzembe wake kwani kwa umahiri alionao isingekuwa rahisi nyavu
zake kutikiswa siku hiyo.
Kiongozi mmoja wa Simba alisema kwamba pamoja na mapungufu yote aliyonayo Kaseja lakini
walikerwa zaidi na kufungwa kwake.
“Hivi unavyomfahamu wewe Kaseja anaweza kufungwa mabao kama yale, kwa
kweli hilo limetacha na maswali mengi kichwani, imetkera sana mwache aende
zake,”alisema
Akienda mbali zaidi, kiongozi huyo alisema ingekuwa vizuri zaidi kama
Kaseja angeweza kuonesha umahiri wake na kuondoa dhana mbovu dhidi yake, lakini
kitendo cha kukubali nyavu zake kutikiswa kilitoa jawabu juu ya maswali
walitokuwa nayo.
Hilo ndilo lilihitimisha mjadala juu ya sababu ya kutemwa kwa Kaseja
ndani ya klabu hiyo aliyochezea kwa mafanikio tangu alipojiunga nayo mwaka 2003
akitokea Moro United.
Hata hivyo, Kaseja ambaye si mzungumzaji sana wa vyombo vya habari
ameendelea kukaa kimya juu ya suala lake hili na jitihada za kumtafuta
ziligonga mwamba baada ya kukataa kuzungumza lolote.
“Dada nakuheshimu sana, lakini kwa sasa sipo tayari kuzungumzia suala
langu na Simba au soka kama una lingine uliza,” alisema Kaseja kwa simu kutoka
kwao Kigoma alipokwenda kwa mapumziko.
HUYU NDIYE JUMA KASEJA
Alizaliwa Aprili 20, 1985 huko Kitongoni, Ujiji mkoani Kigoma akiwa
mtoto wa nne katika Familia ya marehemu Mzee Kaseja.
Amekuwa akiupenda mpira wa miguu tangu akiwa mdogo akirithi kipaji cha
marehemu baba yake ambapo anasema alipata kucheza miaka ya zamani na baba mzazi
wa mchezaji wa Simba ambaye sasa ni kocha wa timu ya Vijana ya Simba, Suleiman
Abdallah Matola.
Alianza kucheza tangu shule ya msingi
hivyo kuchaguliwa katika mashindano ya Taifa (UMITASHUMTA) ambapo huko
ndipo alipong’ara na Mkuu wa Shule ya Sekondari Makongo wakati huo, kanali Idd
Kipingu alimchagua Kaseja pamoja na wachezaji toka sehemu wengvine na
kuwapeleka shuleni hapo kwa ajili ya kuendeleza viopaji vyao.
Baada ya kusukwa kwa karibu miaka minne, alipata nafasi ya kuichezea Taifa
ya vijana wenye umri wa miaka 17 kabla ya kipaji chake kuwavutia viongozi wa
timu ya Moro United na kuichezea mwaka 2001 hadi 2002.
Mwaka 2003 mpaka 2008 aliichezea
Simba kabla ya 2009 kujiunga na mahasimu wao Yanga alipodumu nayo kwa mwaka
mmoja ambapo pia aliiwezesha kutwaa ubingwa wa msimu huo kabla kurejea tena
Simba alipoichezea hadi mwishoni mwa msimu huu.
Mbali na soka Kaseja pia anajihusisha na usajiliamali ambapo anamiliki
duka la nguo lililopo maeneo ya Msasani liitwalo KASEJA Classic Wear.
Comments
Post a Comment