LICHA ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutetea Mkutano
Mkuu wa Julai 13 kugongana na mechi ya kuwania tiketi ya kucheza fainali za
Afrika kwa nyota wa Ligi za Ndani (CHAN), suala hilo limeonekana kugeuzwa nongwa na baadhi ya
wadau.
Jana, baadhi ya wadau walihoji mantiki ya mkutano mkuu
kugongana na mechi hiyo kwa hoja kuwa, mechi hiyo ingeweza kupisha mkutano huo
unaosubiriwa kwa hamu kubwa kutokana na uzito wa agenda zinazotakiwa kujadiliwa
ikiwemo uundwaji wa Kamati ya Maadili.
Hata hivyo, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alitetea
jambo hilo akisema ni kitu cha kawaida kwani
suala la mechi lipo chini ya sekretarieti ya shirikisho hilo ambayo haihusiki na mkutano huo
isipokuwa wajumbe wa mkutano mkuu.
Pamoja na ufafanuzi huo, wadau wameendelea kuibuka wakihoji
kwanini mechi hiyo isifanyike baada ya mkutano huo kwani kwa mujibu wa kanuni
za mashindano ya kimataifa, mechi huweza kuangukia ndani ya siku tatu tofauti.
Ramadhan Hamis na Juma Mnonji ambao ni wanachama wa klabu ya
Simba, walisema serikari inapaswa kuingilia kati kwa kushauri zaidi ili kuweka mambo sawa katika kukwepa
mwingiliano huo kutokana na umuhimu wa mkutano mkuu na mechi hiyo dhidi ya
Uganda itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa.
“Tunadhani si busara mambo haya mawili muhimu kufanyika siku
moja, kwani mechi ingeweza kuangukia siku yoyote kati ya tatu kwa mujibu wa
kanuni za michuano ya kimataifa, hivyo kutoa nafasi ya kutosha kwa wahusika
kujikita zaidi kwenye mkutano na mechi hiyo,” alisema Mnonji akiungwa mkono na
Hamis.
Mnonji amekwenda mbali na kumsihi Rais wa TFF, Leodegar
Chilla Tenga kusikia malalamiko hayo ili
kuondoa kiwingu kilichopo kwani hawaoni haja ya siku hiyo moja kuwa na matukio
hayo mawili makubwa, kwamba mechi inaweza kuchezwa Julai 14.
Wadau wa soka wamekuwa wakiusubiri kwa hamu mkutano mkuu
kutokana na umuhimu wake juu ya mustakabali wa uchaguzi mkuu ambao ulikuwa
ufanyike Februari 24, lakini ukiota mbawa baada ya kuibuka mvutano.
Kwa mazingira hayo, Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa)
limeagiza kuundwa kwa Kamati ya Maadili itakayohusika moja kwa moja,
itakayokuwa ikifanya maamuzi ya kimaadili kwa mujibu wa kanuni za shirikisho hilo .
Comments
Post a Comment