WAAMUZI WATUPWA JELA MIEZI MITATU

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limefungia miezi mitatu waamuzi watatu walioshindwa kuchezesha mechi namba 32 ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) kati ya Mpwapwa Stars ya Dodoma na Machava FC ya Kilimanjaro iliyokuwa ichezwe Juni 2 mwaka huu Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma. 
TFF kupitia Kamati yake ya Waamuzi iliyokutana katika kikao chake cha Juni 12 mwaka huu kupitia taarifa mbalimbali za waamuzi wa RCL ilibaini makosa yaliyofanywa na baadhi ya waamuzi na kuyatolea uamuzi.

Waamuzi hao waliofungiwa ambao wanatoka mkoani Singida ni Jilili Abdallah, Amani Mwaipaja na Theofil Tegamisho. Wamefungiwa kwa kutoripoti katika kituo walichopangiwa (Uwanja wa Jamhuri, Dodoma) na kutoa taarifa ya uongo kwa kushirikiana na Kamishna wa mechi hiyo.

Kanuni iliyotumika kuwafungia ni ya 28 kifungu (d) na (g) ya Ligi za TFF, na adhabu hiyo imeanza Juni 13 mwaka huu. Waamuzi hao pamoja na kamishna badala ya kwenda Uwanja wa Jamhuri, wao walikwenda kwenye Uwanja wa Mgambo ulioko Mpwapwa na kuandika ripoti iliyoonesha kuwa timu ya Machava FC haikufika uwanjani wakati wakijua kuwa mechi hiyo ilitakiwa kuchezwa katika Uwanja wa Jamhuri.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Comments