WAKATI viongozi wa klabu ya Simba wakivutana juu ya usajili
wa kipa wake namba moja, Juma Kaseja (pichani), nyota huyo amelegeza masharti aliyokuwa
ametoa ili aendelee kukipiga Msimbazi.
Habari ambazo Sports Lady Blog imezipata zinasema mgawanyiko huo umejitokeza hivi karibuni
wakati wa kumjadili Kaseja kwa wengi kutaka aongezewe mkataba kama moja la
sharti la nahodha huyo.
Awali, Kaseja alitaka kusainishwa miaka miwili kwa dola
40,000 za Marekani na kuhakikishiwa nafasi yake kama kipa namba moja, masharti
ambayo yalipingwa na baadhi ya viongozi hasa wadau.
Kuna habari kuwa baada ya mazungumzo baina ya uongozi na
Kaseja wameafikiana kumsainisha mwaka mmoja na dau la
sh milioni 30, suala ambalo litatekelezwa ndani ya siku
chache zijazo hasa baada ya mechi ya Juni 16 kati ya Taifa Stars na Ivory
Coast.
Siku hiyo Stars iliyopo kambini itawakaribisha Ivory Coast
kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam katika mechi ya kundi C, katika
kuwania tiketi ya fainali za Kombe la Dunia mwakani.
“Mjadala wa Kaseja tumeshaufunga ingawa hatukuyapa kipaumbele
matakwa yake. Tunasubiri amalize jukumu la kuitumikia Stars, tuingie naye
mkataba mpya,” kilisema chanzo hicho.
Aidha, Simba imeachana na harakati za kumsajili beki wa
kimataifa wa Uganda, Robert Ssenkoom, kwa kutoridhishwa na kiwango chake licha
ya kupewa nafasi hiyo tangu atue nchini Juni 4.
Comments
Post a Comment