Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inaendelea Jumapili (Mei 5 mwaka
huu) kwa mechi moja kati ya Ruvu Shooting na Simba itakayochezwa Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10.15 jioni.
Hiyo itakuwa mechi ya raundi ya 24 kwa timu hizo ambapo
Simba iko nafasi ya nne ikiwa na pointi 39 nyuma ya mabingwa Yanga wenye pointi
57, Azam yenye pointi 48 na Kagera Sugar ambayo ina pointi 40. Ruvu Shooting
iko katika nafasi ya saba ikiwa na pointi 31.
Hadi sasa mabao 348 yameshafungwa katika ligi hiyo huku
Yanga ikiongoza kwa kufunga 45. Polisi Morogoro yenye pointi 22 katika nafasi
ya 12 ndiyo iliyofunga mabao machache ikiwa nayo 13 tu.
African Lyon yenye pointi 19 katika nafasi ya mwisho ndiyo
inayoongoza kwa kuwa na kadi nyingi. Timu hiyo inayofundishwa na Charles Otieno
ina kadi 44 ambapo kati ya hizo nne ni nyekundu. Mtibwa Sugar ya Manungu,
Turiani mkoani Morogoro yenyewe inaongoza kwa kuwa na kadi nyingi nyekundu
ambapo hadi sasa inazo saba.
Comments
Post a Comment