IBF YAMPONGEZA CHEKA KWA KUONESHA KIWANGO CHA JUU KWENYE MASUMBWI


MONDAY 06, MAY, 2013 – DAR ES SALAAM, TANZANIA - Shirikisho la Ngumi la Kimataifa (IBF) limempongeza bondia maarufu wa kitanzania Francis Cheka (pichani)kwa juhudi zake za kuwa bondia mzuri mwenye viwango vya kimataifa katika uzito wa Super Middleweight.
Francis Cheka aliweza kutetea mkanda wake wa IBF Africa uzito wa Super Middle baada ya kumshinda kwa KO bondia Thomas Mashali aka “Simba asiyefugika” tarehe 1 Mei, 2013 katika ukumbi wa PTA jijini Dar Es Salaam. 
IBF inachukua fursa ya kumpongeza Francis Cheka baada ya ushindi huo ambao umedhihirisha kuwa yeye kweli ni bingwa wa bara la Afrika. Francis Cheka atarudiana na bondia wa Malawi Chimwemwe Chiotcha mwezi wa Agusti katika mpambano la kutetea mkanda wake.
Mpambano wao wa marudiano utafanyika katika jiji la Blantyre nchini Malawi na tayari majadiliano ya mpambano huo yanaendelea vizuri. Kampuni ya “Mawenzi Boxing Promotion” ya nchini Malawi chini ya bwana Stephen Mawezni ndiyoitakayoandaa mpambano huo.
Pambano hili linakuja baada ya wadau kadhaa wa ngumi kuomba mabondia hao warudiane walipoonyesha ujuzi mkubwa na ushindani katika mpambano wao Desemba 26 mwaka jana katika uwanja wa Sheikh Amri Abeidi jijini Arusha siku ya Boxing Day.
Baada ya mpambano huo, IBF itampatia Francis Cheka nafasi ya kugombea mkanda wa IBF wa Kimataifa (IBF International Super Middleweight) na mabondia wa Ulaya au Marekani. Hii ni kudhihirisha kuwa Francis Cheka hana tena mpinzanai nchini Tanzania na kumpambanisha na mabondia wa kitanzania ni kumpotezea muda na uwezekano wake wa kutengeneza jina na pesa.
Wakati huo huo bondia Thomas Mashali bado ni bingwa wa Afrika ya Mashariki na Kati (ECAPBF) katika uzito wa Middle kwani mkanda wake haukuwa kati ya mikanda iliyogombewa kwenye mpambano uliomalizika Mei mosi.

Comments