YANGA WAANZA KUINOLEA MSULI SIMBA SC



Wachezaji wa Young Africans wakiwa mazoezi ya GYM jana asubuhi - Quality Centre jijini Dar es salaam
Pamoja na juzi kutangazwa mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2012/2013, kikosi cha timu ya Young Africans jana kimeendelea na mazoezi ya viungo na kujenga misuli (GYM) katika kituo cha mazoezi kilichopo jengo la Quality Cetntre kujiandaa na mchezo dhidi ya Coastal Union siku ya jumatano katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Young Africans ambayo jana imetangazwa rasmi kuwa Mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Vodacom 2012/2013 baada ya timu za Coastal Union na Azam FC kutoka sare ya bao 1-1, imeendelea kujifua kuhakikisha inamalizia mzunguko wa pili wa VPL kwa ushindi kama ilivyofanya tangu kuanza duru la pili.
Azam FC iliyokua na ndoto za kuweza kufikia pointi 56 za Yanga, ilikua ikiombea yenyewe kushinda michezo yake yote mitatu huku iikiombea Yanga kupoteza michezo yake miwili iliyosalia hali ambayo ilikwenda kinyume hapo jana kwa wauza mikate kupata sare ya 1-1 dhidi ya Coastal Union na kuifanya Yanga itangazwe mabingwa wapya wa VPL kwa kuwa na ponti 56 ponti 8 mbele ya Azam yenye pointi 48. 
Huu unakua ni Ubingwa wa 24 kwa Yanga tangu kuanzishwa kwa Ligi Kuu Tanzania bara rekodi ambayo hakuna timu yoyote inayokaribia kufuatia watani wa jadi Simba SC kuwa wametwaa ubingwa huo mara 18 tu. 
Rekodi ya Ubingwa wa Yanga :1968, 1969, 1970, 1971, 1972, 1974, 1981, 1983, 1985, 1987, 1989, 1991, 1992,1993, 1996, 1997, 1998, 2002, 2005, 2006, 2007-2008, 2008-2009, 2010-2011, 2012-2013  
Baada ya kufanya mazoezi katika uwanja wa shule ya sekondari Loyola kwa siku tatu mfululizo kuanzia siku ya jumatano, jana wachezaji waliingia kambini katika hosteli za klabu zilizopo makao makuu mitaa ya Twiga/Jangwani kujiandaa na mchezo wa jumatano.
Kocha Mkuu wa Yanga mholanzi Ernie Brandts amekiongoza kikosi cha wachezaji 26 kufanya mazoezi ya gym leo katika kituo cha Quality Centre ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mchezo unaofuata dhidi ya timu ya Coastal Union siku ya mei mosi jumatano  katika uwanja wa Taifa jijin Dar es salaam.
Yanga imebakisha michezo miwili (Costal Union 01.05.2013) na (Simba SC 18.05.2013) kabla ya kumalizika kwa Ligi Kuu ya Vodaom huku ikiwa tayari imeshatwaa Ubingwa mapema kabla ya kumalizika kwa Ligi Kuu ya Vodacom. 
Uongozi wa klabu ya Yanga unawaomba wanachama, wapenzi na washabiki wa timu ya Yanga kujitokeza kwa wingi siku ya jumatano (mei mosi) katika dimba la uwanja wa Taifa ili kuja kuwashangilia vijana wakiendeleza furaha ya kutwaa Ubingwa wa VPL msimu huu.
DAIMA MBELE, NYUMA MWIKO (DMNM)
EVER FORWARD, BACKWARD NEVER (EFBN) .
CHANZO:www.Youngafricans.co.tz

Comments