YANGA SC UBINGWA HUOOOO

Wafungaji wa mabao mawili ya Yanga leo, Simon Msuva mbele na Nizar Khalfan nyuma wakishangilia. Hapa lilikuwa ni bao la Msuva.


Na Mahmoud Zubeiry
KAMA ni harusi, tayari Yanga wametoa mahari na sasa wanasubiri kwenda kufunga ndoa Mei 1, mwaka huu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumbeba mwali wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Hiyo inafuatia ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya JKT Ruvu Uwanja wa Taifa, hivyo kutimiza pointi 56 na sasa inahitaji pointi tatu zaidi katika mchezo wake ujao dhidi ya Coastal Union ya Tanga ili rasmi kubeba ubingwa, ulioachwa wazi na waliokuwa watetezi, Simba SC.
Pamoja na ushindi, Yanga SC leo iliwapa burudani nzuri mashabiki wake kwa soka maridadi ya kuonana kwa pasi za aina zote, ndefu na fupi, tena kwa staili zote hadi visigino. 
Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Orden Mbaga, hadi mapumziko, Yanga SC walikuwa mbele kwa bao 1-0 lililotiwa kimiani na Simon Msuva, ambaye alifunga kwa ustadi wa hali ya juu.
Mpira uliozaa bao hilo ulianzia kwa Mbuyu Twite ambaye alimrushia mfungaji akawahadaa mabeki wa JKT Ruvu na kuingia kwenye ‘sita’ akifanya kama anataka kutoa pasi, lakini akafumua shuti kali moja kwa moja kufunga.
Hata hivyo, baada ya bao hilo, wachezaji wa JKT Ruvu walimfuata mshika kibendera namba mbili, Lulu Mushi wakilalamikia bao hilo, wakidai lilitokana na maamuzi yasiyo ya haki ya mdada huyo.
Walilalamika mpira waliopewa Yanga warushe walistahili kurusha wao, JKT kwani aliyeutoa ni mshambuliaji wa Yanga, Hamisi Kiiza.
Kipindi cha pili, Yanga SC walirudi na moto zaidi na kufanikiwa kupata mabao mawili zaidi, yaliyofungwa na Hamisi Kiiza dakika ya 59 na Nizar Khalfan dakika ya 64. 
Kiiza alifunga kwa kichwa akiunganisha mpira wa adhabu uliopigwa na David Luhende, baada ya Nizar Khalfan kuchezewa rafu nje kidogo ya eneo la hatari.
Nizar yeye alifunga baada ya kuuwahi mpira uliogonga mwamba na kurudi baada ya Frank Domayo kuunganisha krosi ya Haruna Niyonzima.
Katika mchezo wa leo, Yanga SC iliongozwa na kocha wake Msaidizi, Freddy Felix Minziro ambaye alisema bosi wake, Mholanzi, Ernie Brandts anaumwa Malaria.
JKT iliendelea kuongozwa na Kocha Msaidizi, Azishi Kondo na kocha mpya, Kenny Mwaisabula aliyetarajiwa kuanza kazi leo, hakuonekana uwanjani.
Kikosi cha Yanga SC leo kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’/Said Mohamed dk 86, Mbuyu Twite, David Luhende, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Athumani Iddi ‘Chuji’, Frank Domayo, Haruna Niyonzima, Nizar Khalfan/Said Bahanuzi dk90, Hamisi Kiiza/Jerry Tegete dk82 na Simon Msuva.
JKT Ruvu; Shaaban Dihile, Hassan Kikutwa/Sosstenes Manyasi dk77, Stanley Nkomola, Ramadhani Madenge, Damas Makwaya, Nashon Naftali, Amos Mgisa, Ally Mkanga/Charles Thadei dk78, Mussa Mgosi, Zahor Pazi na Haroun Adolph.

Comments