SIKU chache baada ya
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU), kutowaona na kesi
ya kujibu nyota wanne wa Azam FC, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limesema
kitendo cha uongozi wa klabu hiyo kulifikisha suala hilo katika taasisi hiyo
kilikuwa sahihi.
Azam iliwafikisha
Takukuru wachezaji wake, Deogratius Munishi ‘Dida’, Aggrey Morris, Said Mourad
na Erasto Nyoni kwa madai ya kupokea rushwa ya sh milioni saba kutoka klabu ya
Simba ili wacheze chini ya kiwango.
Kitendo hicho kimekuwa
kikikosolewa na wadau mbalimbali wa soka, kwa madai uongozi wa Azam FC ulikuwa
na uwezo wa kulishughulikia na hata kulifikisha katika vyombo vya kinidhamu vya
TFF.
Akizungumza na Tanzania
Daima jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah,
alisema kwamba Takukuru ndiyo taasisi pekee inayoshughulikia masuala ya rushwa
nchini, hivyo Azam hawakukosea kwenda huko.
“Masuala yote yanayohusu
rushwa, hata katika michezo, Takukuru ndiyo inahusika nayo, hivyo Azam FC
ilikwenda kule kwa mujibu wa taratibu zinazostahili,” alisema.
Kuhusiana na sakata
hilo, ambalo nyota hao watuhumiwa walilifikisha Kamati ya Katiba, Maadili na
Hadhi za Wachezaji, Osiah alisema wachezaji wenyewe wataamua kama watataka
liendelee kuchunguzwa ama la.
Tayari uongozi wa Simba,
chini ya Mwenyekiti wake, Alhaj Ismail Aden Rage, umedai kwenda mahakamani
kuidai Azam fidia ya sh bilioni 1.8 na kuombwa radhi, kwa madai ya kuchafuliwa
kutokana na tuhuma hizo.
Comments
Post a Comment