CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA)
kinasikitika kuwajulisha wadau kuwa bonanza la wanahabari lililopangwa
kufanyika kesho viwanja vya Sigara (TCC) Chang’ombe sasa litafanyika viwanja
vya Leaders Klabu, Kinondoni Dar es Salaam siku hiyo hiyo ya Aprili 6,2013.
Uamuzi huo wa kushtukiza umefikiwa kwenye kikao cha dharura
kilichofanyika jana usiku kati ya TASWA ambao ni waandaaji na wadhamini wa
bonanza hilo Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kutokana na kushindwa kuafikiana
baadhi ya mambo na menejimenti ya viwanja hivyo.
Tunawaomba sana radhi wanahabari kwa usumbufu mkubwa ambao
wataupata kutokana na mabadiliko haya, lakini tunaamini yamefanyika kwa dhamira
nzuri yenye nia ya kuboresha bonanza letu na kwa kiasi kikubwa litafana kwa
asimilia 100.
Dhamira ya TASWA ni
kuona inakuwa na bonanza zuri lisilokuwa na aina yoyote ya kwikwi, hivyo tayari
tumeshamalizana na menejimenti ya viwanja vya Leaders Klabu na kila kitu
kitakuwa safi kuliko maelezo.
Pia tunaishukuru menejimenti ya viwanja vya Sigara kwa
ushirikiano iliotupa kwa nia ya kufanya bonanza hilo eneo lao, ingawa ndoto
zetu hazikutumia, lakini tunaamini siku za usoni tunaweza kufanya nao kazi.
Tunasisitiza lengo la bonanza letu ambalo mgeni rasmi
atakuwa Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe ni kuwaweka pamoja waandishi
wote wa habari bila kujali ni wa siasa, michezo, uchumi, afya na mambo mengine
pamoja na wafanyakazi wa vyombo mbalimbali vya habari, ili kubadilishana mawazo
na kufurahi pamoja.
Awali bonanza letu ilikuwa lifanyike Leaders Klabu, lakini
tulilihamishia viwanja vya Sigara kutokana na wadau wengi kuomba wapate nafasi
ya kwenda kutazama mechi ya Kombe la Shirikisho kati ya Azam ya Tanzania na
Barrack Young Controllers ya Liberia kesho. Hata hivyo tunaamini wahariri wa
habari za michezo watajipanga vizuri kulingana na mabadiliko hayo na hakuna
litakaloharibika.
Pia katika kuboresha bonanza hilo litakalotumbuizwa na bendi
ya Extra Bongo na kundi la taarabu la Jahazi Modern, kutafanyika mchezo wa soka
kati ya wanahabari ambao wameoa na wale ambao hawajaoa utakaofanyika baada ya
michezo ya kawaida baina ya vyombo vya habari kumalizika.
Bonanza litaanza saa tatu asubuhi kwa washiriki kucheza
michezo mbalimbali ikiwemo soka, netiboli, wavu, kuruka kichura, aina mbalimbali
za riadha, kuvuta kamba na kucheza muziki. Bonanza litamalizika saa moja usiku.
Ahsanteni.
Amir Mhando
Katibu Mkuu TASWA
05/04/2013
Comments
Post a Comment