SIMBA SPORTS CLUB
25/04/2013
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
UONGOZI wa Simba umekubaliana na hatua ya
serikali kuzuia kuchezwa kwa mchezo uliopangwa kuchezwa leo wa Ligi Kuu ya Tanzania baina
ya Wekundu wa Msimbazi na Ruvu Shooting Stars.
Hata hivyo, uongozi wa Simba
haujafurahishwa na namna uzuiaji huo ulivyofanyika. Taarifa imetolewa leo
kwenye siku ya mechi yenyewe wakati maandalizi yote yakiwa yamefanyika na hivyo
kusababisha matatizo katika sehemu kubwa tatu.
Mosi, uongozi wa Simba umeingia gharama
kubwa ya kuweka timu kambini na kujiandaa na mechi. Pili, benchi la ufundi na
wachezaji walikuwa tayari wamejiandaa na mechi kimwili na kiakili na
kuahirishwa huku kwa mechi kumesaidia tu kuvuruga programu. Tatu, wapenzi na
washabiki wa Simba wamepata usumbufu wa kwenda uwanjani na kukuta hakuna mechi.
Uongozi wa Simba unapenda kutumia nafasi
hii, katika namna ya kipekee kabisa, kuwaomba radhi wapenzi na wanachama wake
ambao walifika Uwanja wa Taifa kutazama mechi ambayo haikuwapo.
Washabiki ndiyo wanaoifanya Simba na mchezo
wa mpira wa miguu nchini uwe na umaarufu ulionao na bila wao ligi yetu inaweza
kupoteza nguvu na ushindani ilionao.
Tunashauri pia kwamba siku za mechi ambapo
Ligi Kuu inachezwa (match days), inatakiwa kuwa zinafahamika na isiwe kila siku
mechi zinachezwa. Simba ilikuwa na mechi wikiendi iliyopita na Ruvu ilikuwa na
mechi Mbeya zaidi ya wiki moja iliyopita na hivyo mechi hii ingeweza kuchezwa
hata jana (Jumatano) ambayo ni siku ya kawaida kwa mechi kuchezwa badala ya leo
Alhamisi.
Ni matumaini yetu kwamba kuahirishwa kwa
mechi hii kutakuwa fundisho kubwa katika upangaji wa ratiba na uahirishaji wa
mechi ambao una faida kwa pande zote husika.
Comments
Post a Comment