Rais wa Shirikisho
la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga ametoa mipira zaidi ya 1,200
yenye thamani ya dola 30,000 za Marekani kwa vyama vya mpira wa miguu vya mikoa
ya Tanzania Bara na vituo 21 vilivyo hai vya kuendeleza vijana
(academies).
Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) lilimpa
Rais Tenga fedha hizo ikiwa ni shukrani kwake kwa kushughulikia mgogoro wa
uongozi wa mpira wa miguu nchini Kenya uliodumu kwa miaka miwili; ambapo nchi
hiyo kutokana na mgogoro huo ilikuwa na vyama viwili (KFF na FKL).
Akizungumza katika hafla ya kukabidhi mipira hiyo kwenye
ofisi za TFF, Dar es Salaam leo (Aprili 22 mwaka huu), Rais Tenga amesema
amefanya hivyo kwa vile anaamini kuwa mipira ndiyo kitu muhimu katika kuinua
mchezo huo mahali popote.
“Dhamira yangi si kushukuru kwa hafla hii, bali kutoa
sababu kwa nini nimefanya hivi. Ninaamini kwa kuanzia mipira ndiyo muhimu, pili
kwa kufanya hivi itaonekana kweli mipira imegawiwa,” amesema Rais
Tenga.
Amesema amesema mpira wa miguu kwa Tanzania unahitaji
sana watu wa kujitolea, na yeye amefanya hivyo kwa kujitolea kutokana na ukweli
shughuli anazotumwa na FIFA ni za kujitolea.
Rais Tenga ambaye pia alitumwa na FIFA kutatua matatizo
ya uongozi wa mpira wa miguu katika nchi za Uganda, Zambia na Sudan Kusini
amesema anaamini anapata fursa hizo kutokana na kuwa kiongozi wa TFF, na kwa
kuwakumbuka waliomchagua ndiyo maana hakusita kupeleka fedha hizo kwenye
mipira.
Amesema moja ya ndoto zake wakati anaingia kuongoza TFF
mwaka 2004 ameshindwa kutimiza ni kusaidia mipira, kwani uwezo wa kununua mipira
kwa wanaocheza katika ngazi ya chini hasa watoto haupo.
“Hizi kelele zote za maendeleo ya mpira wa miguu ni kwa
sababu shuleni hakuna vifaa. Nia yangu ilikuwa shule zote zipate mipira, lakini
hiyo ni moja ya ndoto nilizoshindwa kutekeleza. Vipaji haziwezi kupatikana kama
watoto hawachezi.
“Tunashukuru sana kwa Serikali kurejesha mpira shuleni.
Hata nitakapoondoka madarakani nikipata nafasi nitaendelea kuomba mipira kwa
ajili ya shule,” amesema Rais Tenga.
Vyama vya mikoa ambavyo jumla ni 32 (Tanzania Bara na
Zanzibar) kila kimoja kimekabidhiwa mipira 25 (kumi saizi namba tano, 15 saizi
namba nne kwa ajili ya vijana). Kwa academies ambazo ni 21 kila moja imepewa
mipira 25 (minane saizi namba tano, na 15 saizi namba nne).
Viongozi waliohudhuria hafla hiyo ni Mwenyekiti wa Chama
cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) Almasi Kasongo, Katibu wa Chama
cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mwanza (MZFA) Nassib Mabrouk na Katibu wa Chama cha
Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) Riziki Majala.
Kwa upande wa shule alikuwa Kanali mstaafu Idd Kipingu
ambaye ni mmiliki wa shule ya Lord Baden ya Bagamoyo mkoani Pwani.
Comments
Post a Comment