Mechi tano kati ya sita za Super Week za Ligi Kuu ya
Vodacom zilizokuwa zioneshwe moja kwa moja (live) na Kituo cha televisheni cha
SuperSport cha Afrika Kusini sasa hazitaoneshwa kutokana na matatizo ya
kiufundi.
Kwa mujibu wa
Mtayarishaji Mtendaji (Executive Producer) wa SuperSport Kanda ya Afrika, Max
Tshunungwa ambaye yuko nchini, wameshindwa kuonesha mechi hizo kutokana na
matatizo ya kiufundi katika magari yao ya kurushia matangazo (OB van)
yanayohudumia Afrika Mashariki- Kenya, Tanzania na Uganda.
Mechi hizo ni kati ya Azam na African Lyon, Yanga na
Oljoro JKT, Azam na Simba, Coastal Union na JKT Ruvu na Mgambo Shooting na Yanga
itakayochezwa Aprili 17 mwaka huu jijini Tanga.
Tatizo hilo pia limeathiri mechi za Ligi Kuu ya Kenya
(KPL) ambazo hazitaonekana wikiendi hii. SuperSport ndiyo yenye haki za
matangazo ya televisheni kwa ligi hiyo ya Kenya.
Tshunungwa amekutana na Sekretarieti ya TFF na Kamati ya
Ligi kuelezea tatizo hilo. SuperSport kwa kushirikiana na Kamati ya Ligi na TFF
watapanga mechi nyingine za Super Week kabla ya ligi kumalizika msimu
huu.
Pia TFF, Kamati ya Ligi na SuperSport watakuwa na
mkutano mfupi wa waandishi wa habari wakati wa mapumziko kwenye mechi ya leo
kati ya Yanga na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Taifa.
Comments
Post a Comment