MASHABIKI WA MAN U MOROGORO WAANDAA 'PARTY' LA KUSHEREHEKEA UBINGWA


Na Daudi Julian, Morogoro
Mashabiki wa timu ya soka ya Manchester United ya England wa mkoani Morogoro wameandaa hafla maalum kwa ajili ya kuipongeza timu hiyo kwa kutwaa ubingwa wa ligi kuu nchini humo. 
Akizungumza na mtandao huu mjini hapa, mratibu wa hafla hiyo iliyopewa jina la ‘Moro Man U Festival’, Mangi Chang’waro alisema maandalizi yanakwenda vizuri na kwamba hafla hiyo itafanyika mara tu baada ya kumalizika kwa ligi kuu ya England. 
Chang’waro alisema lengo la hafla hiyo ambayo ni ya kwanza kufanyika mkoani hapa ni kuipongeza timu hiyo kwa kutwaa ubingwa na pia kuwakutanisha pamoja mashabiki wa Manchester United mkoani Morogoro. 
Alisema siku hiyo mashabiki hao wanatakiwa kufika wakiwa ndani ya jezi ya Man U na kwamba michezo mbalimbali ya timu hiyo itaonyeshwa katika screen kubwa . 
“Maandalizi ni mazuri na tayari tumeshaanza kusambaza kadi za mwaliko kwa mashabiki na niseme mwitikio ni mzuri’, alisema. 
Alisema mashabiki hao watatumia hafla hiyo kusherehekea ubingwa pamoja, kutambuana, kupongezana, kunywa, kula na kucheza muziki. 
Man U ilitangaza ubingwa hivi karibuni baada ya kuichapa Aston Villa mabao 3-0 yaliyofungwa na Robin van Persie.
 

Comments