YANGA NA KAGERA YAINGIZA MILIONI 77

Frank Domayo wa Yanga akimiliki mpira huku akidhibitiwa na kiungo wa Kagera katika mechi hiyo.

Na Boniface Wambura
WATAZAMAJI 13,398 wameshuhudia pambano la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kati ya Yanga na Kagera Sugar lililochezwa juzi (Februari 27 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kuingiza sh. 77,117,000.
Mechi hiyo namba 130 iliyochezeshwa na Simon Mberwa kutoka mkoani Pwani ilimalizika kwa Yanga ambao wanaongoza VPL wakiwa na pointi 42 kuibuka na ushindi wa bao 1-0 lililofungwa dakika ya 45 na Haruna Niyonzima.
Viingilio vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 18,291,297.95 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 11,763,610.17.
Kiingilio cha sh. 5,000 ndicho kilichovutia watazamaji wengi ambapo waliokata tiketi hizo walikuwa 11,908 na kuingiza sh. 59,540,000 wakati idadi ndogo ya washabiki ilikuwa ya kiingilio cha sh. 20,000 kilichovutia washabiki 80 na kuingiza sh. 1,600,000.
Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 9,300,659.97, tiketi sh. 3,348,990, gharama za mechi sh. 5,580,395.98, Kamati ya Ligi sh. 5,580,395.98, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 2,790,197.99 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 2,170,153.99.
Wakati huo huo: Ligi Kuu inatarajiwa kuendelea kesho kwa Polisi Morogoro kuikaribisha Oljoro JKT ya Arusha kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
Hata hivyo, timu hizo haziko katika kinyang’anyiro cha kuwania ubingwa ambapo Yanga ndiyo inayoongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 42 wakati Oljoro JKT inayofunzwa na Alex Mwamgaya ikiwa nazo 21 na Polisi Morogoro pointi 15.
Oljoro JKT iko katika nafasi ya tisa. Polisi Morogoro ambayo katika mzunguko wa pili imebadilika ikiwa chini ya Kocha Adolf Rishard inashika nafasi ya 12 ikiziacha mkiani Toto Africans yenye pointi 14 na African Lyon ambayo ina pointi 13.
Ligi hiyo itaendelea Jumatano (Machi 6 mwaka huu) kwa mechi kati ya Oljoro JKT vs Tanzania Prisons (Sheikh Kaluta Amri Abeid), African Lyon vs Ruvu Shooting (Azam Complex, Chamazi) na Mgambo Shooting vs Mtibwa Sugar (Mkwakwani) wakati Machi 7 mwaka huu ni JKT Ruvu vs Kagera Sugar (Azam Complex, Chamazi).
Machi 9, mwaka huu kutakuwa na mechi mbili; Yanga vs Toto Africans Uwanja wa Taifa), na Azam vs Polisi Morogoro (Azam Complex, Chamazi).

Comments