TIMU ya Yanga imezidi
kuyoyoma kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Tanzania bara, baada ya leo kushinda bao 1-0 dhidi
ya maafande wa Ruvu Shooting ya Pwani katika mechi kali iliyochezwa kwenye
Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Kwa ushindi huo, Yanga sio tu
imeendeleza rekodi yake ya kutofungwa tangu kuanza raundi ya pili ya ligi hiyo,
Januari 26, pia imezidi kuukaribia ubingwa wa ligi hiyo iliyoanza Septemba 15,
mwaka huu.
Yanga sasa inaongoza ligi
hiyo yenye timu 14 kwa pointi 48 ilizovuna katika mechi 20 ikifuatiwa na Azam yenye pointi 37 na
mabingwa watetezi Simba wakiwa nafasi ya tatu kwa pointi 34, wakiwa nyuma kwa
mchezo mmoja dhidi ya Yanga.
Katika mechi ya leo,bao
pekee lililopeleka pointi tatu Jangwani, lilifungwa dakika ya 48 na nyota wake wa kimataifa wa
Uganda, Hamis Kiiza akimalizia krosi
maridadi ya Nizar Khalfan.
Comments
Post a Comment