TFF YAOMBOLEZA KIFO CHA ATHUMAN KILAMBO


Shrikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha mchezaji wa zamani wa timu ya Yanga, Pan Africans na Taifa Stars, Athuman Kilambo kilichotokea jana (Machi 10 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.
Msiba huo ni mkubwa kwa wadau wa mpira wa miguu kwani kwa nyakati tofauti Kilambo akiwa mchezaji, na baadaye kocha alitoa mchango mkubwa kwa timu mbalimbali alizochezea na kufundisha zikiwemo Pan Africans na Cargo, hivyo mchango wake tutaukumbuka daima.
TFF inatoa pole kwa familia ya marehemu Kilambo, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) na klabu ya Pan Africans na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.
Maziko yanatarajiwa kufanyika leo (Machi 11 mwaka huu) katika makaburi ya Kisutu mkoani Dar es Salaam ambapo TFF imetoa ubani wa sh. 100,000. Mungu aiweke roho ya marehemu Kilambo mahali pema peponi. Amina
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Comments