SIMBA SC:MKUTANO WA KESHO NI BATILI


KUMEKUWAPO na taarifa za kufanyika kwa Mkutano Mkuu wa Wanachama wa Simba uliopangwa kufanyika Kesho (Machi 17, 2013) jijini Dar es Salaam kujadili mustakabali wa klabu.
Ikumbukwe kwamba Mkutano Mkuu wa Wanachama ndiyo chombo cha juu kabisa cha maamuzi kwa klabu yetu. Katiba ya Simba SC imeupa Mkutano Mkuu hadhi ya juu mno na ndiyo maana imeweka utaratibu wa kufanyika kwake.
Miongoni mwa utaratibu ni kwamba ni lazima uitishwe na Mwenyekiti aliye madarakani wa klabu. Kwa kushirikiana na Kamati ya Utendaji, ndiye atakayepanga ajenda, mahali na wakati wa kufanyika kwa mkutano wenyewe.
Katika miaka ya nyuma, zilikuwepo nyakati ambapo klabu ilikaa hadi miaka mitatu pasipo kuitishwa kwa Mkutano Mkuu wowote wa wanachama. Hakuna mwanachama au kikundi chochote kilichojitokeza kudai mkutano wa dharura wakati huo ingawa ilikuwa ikifahamika kwamba huo ulikuwa ni ukiukwaji mkubwa wa katiba ya klabu.
Tangu uongozi huu uingie madarakani takribani miaka mitatu iliyopita, mikutano mikuu miwili ya wanachama imefanyika kwa mujibu wa KATIBA. Mungu akijaalia, uongozi huu utafanya mkutano mwingine wa kawaida wa wanachama baadaye mwaka huu.
Hata hivyo, kwa kuzingatia hali halisi ya klabu, Mwenyekiti wa Simba, Alhaji Ismail Aden Rage (Mb), mwezi uliopita alitangaza dhamira yake ya kuitisha Mkutano Mkuu wa Dharura wakati wowote kuanzia sasa.
Rage alisema mkutano huo ungekuwa na ajenda moja tu; Kujadili Mwenendo wa Klabu kwenye mashindano inayoshiriki msimu huu.
Kwa bahati mbaya, Mwenyekiti alishikwa na maradhi na akapelekwa India kwa matibabu na yuko huko hadi Mola atakapomjalia afya njema na kurejea. Kuna uwezekano mkubwa, Inshallah, akarejea mwishoni mwa wiki ijayo.
Hii maana yake ni kwamba uongozi umeridhia kufanyika kwa Mkutano wa wanachama. Kimsingi, kama uongozi umeridhia, hakuna mwanachama mwingine anayeweza kuitisha mkutano mkuu mwingine.
Mwenyekiti ameruhusiwa kuitisha Mkutano Mkuu kwa sababu alichaguliwa na wanachama na hivyo ana nguvu ya kisheria (locus standi) kufanya hivyo. Hawa wengine wanaoitisha mkutano wana nguvu gani ya kisheria kufanya hivyo? Walichaguliwa na nani kuwakilisha wanachama? Lini na wapi?
Uongozi pia unaweza kuitisha mkutano kwa vile wenyewe ndiyo wenye leja ya wanachama. Klabu sasa ina database yake ya kompyuta inayotambua wanachama walio hai na wasio hai.
Kwa kutumia database hiyo, uongozi huu unatambua wanachama walio hai na wasio hai. Hakuna mtu mwingine yeyote, aliye nje ya uongozi huu anayefahamu wanachama walio hai na wasio hai. Hao wanachama wanaoitana kufanya mkutano, wamehakikiwa na nani kubaini uhalali wao huo?
Uongozi wa Simba SC unaona kwamba wale wanaolazimisha kufanyika kwa Mkutano Mkuu wana ajenda binafsi na si za maslahi ya klabu. Kama kweli wangekuwa na nia njema na klabu wangesubiri mkutano ambao utaitishwa punde.
Kwani, kuna uharaka gani wa kufanyika mkutano kesho? Kwanini hawataki Mwenyekiti, ambaye wanachama walimpa mamlaka ya kuongoza klabu kwa kipindi cha miaka minne, awepo kwenye mkutano huo?
Kwanini hawataki kuungana na wana Simba wengine kumwombea Mwenyekiti kwa Mungu ili amwepushe na ugonjwa na kumrejesha salama hapa nyumbani? Kwanini mikutano hii iitishwe katika kipindi ambacho uongozi umefungua mikono yake na kukaribisha kila mmoja mwenye mapenzi mema na klabu kuja kuchangia?
Kwenye macho ya Katiba ya Simba na sheria za Tanzania, huu mkutano wa kesho ni batili na una lengo la kuleta vurugu na mifarakano kwenye jamii na michezo kwa ujumla wake. Michezo ni amani na furaha na michezo si vurugu.
Tayari uongozi wa Simba umetoa taarifa kwa Jeshi la Polisi na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuhusiana na ubatili wa mkutano huo. Tunapenda kuwaomba wanachama wetu wasiopenda fujo na vurugu kwenye michezo kukaa mbali na mkutano huo kwa vile vyombo vya dola vitaufuatilia.
Uongozi hautajiingiza katika kutoa dhamana au msaada wa namna yoyote kwa yeyote ambaye atachukuliwa hatua na vyombo vya dola kutokana na kujihusisha na mkutano huo.
Pia, Simba SC inatoa wito kwa vyombo vya habari kuwa makini wakati vinaporipoti matukio ya vurugu kwenye michezo. Kabla mtu hajahojiwa kujieleza kama mwanachama wa Simba, ni vema kwanza akaonyesha kadi yake ya uanachama na risiti za malipo yake.
Wakati mwingine, waandishi huwa tunawapa nafasi kwenye vyombo vyetu vya habari watu ambao hawana mchango wowote kwenye kukuza michezo bali kuleta vurugu. Kwanini, tungejiuliza, ni watu wale wale ambao kila mwaka huonekana wakati wa vurugu na wakati wa amani huwa hawaonekani?
Kwanini, vyombo vyetu vinatoa nafasi kwa watu ambao lengo lao ni kuhakikisha vilabu vyetu vinazidi kubaki nyuma, vinakuwa na vurugu kila wakati na michezo inaonekana kama ni sehemu ya wahuni na watu wasio na utaratibu?
Mpira bado haujaleta tija kubwa kwenye uchumi wa Tanzania na kunufaisha wachezaji kwa sababu baadhi ya watu makini na makampuni makubwa yanaogopa kujiingiza kwenye michezo kwa sababu ya tabia kama hizi.
Ni vema vyombo vya habari vikafanya jitihada kubwa katika kuwatambua waleta vurugu, si katika klabu ya Simba pekee, bali kwenye sekta ya michezo kwa ujumla, ili visiwape nafasi ya kuharibu na badala yake vitoe nafasi kwa wale wenye lengo la kujenga.
Tunasisitiza, uongozi huu utaitisha Mkutano Mkuu wa Wanachama Wote mara baada ya kurejea kwa Mwenyekiti.

Comments